July 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Junior Patrol inavyosaidia kupunguza ajali kwa wanafunzi

Na Penina Malundo, Timesmajira

AJALI za Barabarani ni tatizo nchini, ambayo unasababishwa na miundombinu mibovu na ujenzi holela usiozingatia ramani ya mipango miji katika maeneo mengi ya miji.

Asilimia kubwa ya maeneo yenye miji ikiwemo jiji la Dar es Salaam unachangia kwa kiasi kikubwa uwepo wa ajali za barabarani kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo Ongezeko la vyombo vya moto mjini pamoja na watu.

Mbali na Ongezeko la magari mengine mjini pia Shule nyingi za sekondari na Msingi asilimia kubwa zimejengwa pembezoni mwa barabara hususani zilizopo katikati ya miji.

Kutokana na kukithiri kwa ajali za barabarani,Kundi la Wanafunzi linatajwa kuwa ni miongoni mwa kundi linaloguswa na tatizo la ajali za barabarani ukizingatia nao ni watumiaji wakubwa wa barabara.

Ujenzi wa shule hizo zilizojengwa pembezoni mwa barabara, hali itakayohatarisha maisha ya wanafunzi katika shule hizo katika kupata ajali kipindi wanapovuka barabara au wanapokatiza barabarani.

Ili kuweza kupunguza kasi za ajali barabarani kwa wanafunzi wanaosoma shule hizo zilizopo karibu na barabara zinapaswa kuwa na mikakati maalum ya kusaidia jamii katika kupambana na wimbi ya ajali barabarani na uboreshaji wa hali ya Usalama Barabarani nchini.

Miongoni mwa mikakati ni pamoja na kuendeleza mafunzo ya watoto katika kusaidiana kuvuka barabara kwa kutumia vibao maalum (Scholar Junior patrol),Kufundisha walimu namna ya kufundisha wanafunzi somo la usalama barabarani, Kusimamia na kuhakikisha watoto wanavushwa barabarani,Kufanya ukaguzi ili kuhakikisha elimu ya usalama barabarani inatolewa mashuleni, Kuchukua hatua za kisheria dhidi ya wanaokaidi na kutokutii alama za barabarani na Watoto kuwa na uelewa wa elimu ya usalama barabarani na kuwa salama zaidi watumiapo barabara.

Hii itasaidia lengo la Tatu la Malengo ya endelevu ya millennia ambalo linalenga kupunguza idadi ya vifo na majeruhi vitokanavyo na ajali za barabarani ifikapo mwaka 2020 na nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania zipo kwenye harakati za kutekeleza lengo hilo la tatu na kuhakikisha ajali za barabarani zinapungua kwa kiasi kikubwa.

Katika lengo la mwongo namba nne inaelezea watumiaji wa barabara na tabia za watumiaji barabarani huku namba moja inasema uongozi katika barabara pamoja na uinjinia wake katika kuhakikisha kunakuwa na usalama wa barabara.

Usalama barabarani, ni moja kati ya mambo yanayotiliwa mkazo sana na Shirika la afya duniani(WHO) halikadhalika Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia ,Wazee na Watoto.

Kwa mujibu wa WHO watu milioni 1.24 wanakufa kila mwaka kutokana na ajali za barabarani, watu millioni 1.9 wapo kwenye uwezekano mkubwa wa kufa ifikapo mwaka 2030 kama hatua madhubuti hazitochukuliwa.

Katika ripoti yaGlobal Status ya WHO inayohusiana na masuala ya usalama barabarani inaonyesha kwamba watu milioni 1.3 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na ajali za barabarani, hata hivyo ripoti hiyo inaeleza kwamba kati ya watu 20 hadi 50 wanaachwa na majeraha na kiasi cha dola 1.8 trillioni zinapotea kila mwaka na kusababisha kushuka kwa uchumi.

Katika malengo endelevu ya milenia lengo namba 11.2 linaeleza bayana kuwepo na mipango miji ya uhakika, miundombinu bora na salama ifikapo mwaka2030 ili kuwa na uhakika wa usalama barabarani kwa watumiaji wa barabara.Miongoni mwa mipango hiyo ni pamoja na kuhakikisha kunakuwepo na vivuko vya watembea kwa miguu barabarani,kuchorwa kwa mistari ya pandamilia katika sehemu za vivuko pamoja na uwekaji wa matuta katika maeneo ya shule.

Hali hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa Wanafunzi hususani watoto kupunguza kugongwa na magari katika maeneo hayo.

Aidha upunguzwaji wa mwendokasi katika maeneo ya Shule na makazi ya watu kwa kuokoa maisha ya watoto wanasoma shuleni pembezoni mwa Barabara.

Tatakwimu za ajali za barabarani zinaonyesha Mwaka 2017,watoto wa umri kati ya miaka saba hadi 12 jumla ya watoto 60 walifariki dunia na waliojeruhi wakiwa 230 ,huku kwa mtoto wa mwaka mmoja hadi miaka saba takwimu inaonyesha kuwa jumla ya watoto 11 walifariki dunia na waliojeruhiwa wakiwa 143 huku watoto wenye umri kati ya miaka 13 hadi 18 waliofariki walikuwa watoto 223,hii imefanya kuwe na jumla ya watoto 294 waliofariki na waliojeruhiwa ni takribani watoto 832 kwa mwaka huo.

Katika kipindi cha mwaka 2018 watoto wadogo kati ya umri wa mwaka mmoja hadi saba jumla ya watoto wanne walikufa huku kwa umri wa miaka saba hadi 12 waliokufa walikuwa watatu walifariki na watoto kati ya umri wa miaka 13 hadi 18 takribani watoto 73 na kufanya jumla ya watoto 94 kufariki na waliojeruhi kuwa 258.

Huku kwa Mwaka 2019,takwimu inaonyesha watoto wa umri kati ya umri wa mwaka mmoja hadi saba hakukuwepo na kifo,watoto kati ya umri wa miaka Saba hadi 12 walifariki watoto 10 huku watoto kati ya umri wa miaka 13 hadi 18 takribani watoto 42 walifariki dunia na kufanya jumla ya watoto waliofariki kwa mwaka huo kuwa 52 na kujeruhiwa watoto 177.

Hivyo utumiaji wa Junior Patrol katika shule mbalimbali utaweza okoa maisha ya watoto wengi na kuhakikisha usalama wa barabarani unazingatiwa na kuhakikisha unalinda kundi la watoto hususani Wanafunzi ambao wahanga wakubwa wa ajali hiyo.

Hii ni sehemu ya program ya Shirika la Afya Duniani (WHO )kwa kushirikiana na Kituo cha Kimataifa cha Waandishi wa Habari(ICFJ )katika kuhakikisha watoto wanalindwa wanapokuwa barabarani.

Mmoja wa WAnafunzi wa Shule ya Msingi Mnadani,Mwajuma Juma anasema programu ya Junior Patrol imekuwa mkombozi kwao katika kuwavusha barabara pindi wanapoingia shuleni au wanapoenda majumbani mwao .

Anasema programu hiyo imekuwa msaada Mkubwa kwao kwani wwalikuwawakipata changamoto muda wa kuvuka barabarani kwani magari mengine yanashinda kusimama ili wao wavuke.

Jumaa anasema mara nyingi watu wengi wanakuwa hawapo makini wakiwa wanatembea kwa miguu au wakiwa wanaendesha magari kwa kuchezea simu wakati wakiwa barabarani au wakati mwingine watu kutovuka katika mistari ya pundamilia.

“Utakuta mtu anatembea barabarani huku anachezea simu wakati mwingine mtu anavuka barabara havuki kwenye zebra pia wapo watoto wenzetu wanaocheza barabarani ambapo ni hatari kwa afya yao,”anasema

Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mnadani ,Fidelis kaishori anasema wanafurahia programu ya Junior Patrol kwa wanafunzi wao kwani inaenda kuokoa kundi kubwa lililokuwa linapata ajali pindi wa wanafunzi wanapovuka barabara.

” Shule yetu ipo barabarani na wanafunzi wanatoka upande wa pili wa barabara hivyo elimu hii itawasaidia na inaendeleaje kuwasaidia watoto kuvuka Barabara kutoka nyumbani kuja shuleni na kutoka shuleni kwenda nyumbani,”anasema na kuongeza

“Watoto wetu wameshakuwa wahanga wa ajali kwani tayari wameshagongwa wanafunzi watatu kupitia elimu hii sasa watasaidia kuwavusha wenzao na kuwa na uelewa zaidi juu ya usalama barabarani, “anasema a

Aidha Meneja Mkuu wa Taasisi ya Masuala ya Usalama Barabarani ijulikanayo kwa jina la Amend ,Simon Kalolo anasema junior patrol inasaidia kwa shule na inakuwa mlinzi kwa watoto pindi wanapoingia shuleni au muda wa mapumziko wanapokuwa wanatoa inasaidia kusimamisha magari.

Anasema watoto wadogo waliopo darasa la kwanza na la pili ni wahanga wakubwa wa ajali barabara hivyo vibao hivyo vinakuwa saidizi kwa watoto hususani kwa mtu anaepatiwa mafunzo na vitendea kazi ya kuhakikisha wanasimamisha magari na wenzao wanapovuka.

“Ni vema msimamisha magari akiwa na makoti ya kuhakisi Mwanga,vibao vya kusimama na kwenda wanapopatiwa na kufanyiwa mafunzo itasaidia kupunguza matukio ya ajali kuendelea kutokea katika maeneo ya shue,”anasema na kuongeza

“Tusiruhusu hizi Junior patrol pekee yake bila kuruhusu miundombinu rafiki kwamba tumeona baadhi ya maeneo watoto wanavushwa lakini miundombinu sio rafiki hakuna matuta ya kupunguza mwendo vyombo vya moto, hakuna vivuko rasmi vya kuruhusu watoto wavuke na watu wazima wavuke katika eneo hilo pia hakuna alama ,”anasema na kuongeza

“Sio uwepo wa Junior Patrol pekee yake ni vema kuimarisha miundombinu yetu ambayo ni rafiki ya kutahadharisha watu ambayo itahakikisha na kulinda uhai wa watu ,”anasema

Aidha anasema watoto wanapaswa kuendelea kupata elimu ya usalama barabarani na walimu wao huku madereva nao waendelee kukumbushwa juu ya ufataji wa Sheria muhimu za usalama barabarani.