March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jeshi la Polisi Nchini lajipanga kwa ujio mkubwa wa Watalii baada ya uzinduzi wa Royal Tour

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online, Arusha

Jeshi la Polisi nchini limejipanga vyema kuimarisha ulinzi na usalama baada Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuzindua filamu ya The Royal Tour hivi karibuni kwa lengo la kuutangaza utalii.

Akitoa taarifa hiyo kwa niaba ya msemaji wa Jeshi la Polisi Nchini, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP JUSTINE MASEJO amesema Jeshi la Polisi Nchini limeanzisha kitengo maalumu cha Utalii na Diplomasia ambacho kipo kwa ajili ya kuwahudumia Watalii na Wanadiplomasia wanaofiika nchini.

Aliendelea kusema Mkoa wa Arusha ambapo ni kitovu cha utalii nchini kumeanzishwa kituo cha Polisi maalumu kwa ajili ya kuhudumia Watalii na Wanadiplomasia ambapo Askari wake wamewapatiwa mafunzo ndani na nje ya Nchi namna bora ya kuhudumia watalii.

Pia amesema kuwa kuna magari maalumu ambayo hutumiwa na kituo hicho kwa ajili ya doria mbalimbali ikiwemo kwenye vivutio vya utalii, hoteli za kitalii pamoja na maeneo mengine ambayo wageni hupenda kutembelea.

Sambamba na hilo amesema kuwa kuna vituo vidogo vya Polisi vilivyopo katika wiliya ya Arumeru, Monduli, Longido, na Karatu ambapo magari ya utalii hufika kwa ajili ya kupata taarifa za kitalii pamoja na ukaguzi wa usalama wa magari hayo.

Alimaliza kwa kusema kuwa Jeshi la Polisi Nchini litaendelea kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan katika kuutangaza utalii kwa kuboresha mazingira ya kiusalama kwa watalii wanaofika nchini.