Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi, imewataka wananchi wa mikoa 15 inayotekeleza zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika mzunguko wa kwanza wa awamu ya pili kuzitumia siku chache zilizobaki katika mikoa yao kuhakikisha wanajitokeza kujiandikisha na kuhakiki taarifa zao ili wasijekosa haki yao ya msingi ya kupiga Kura katika uchaguzi ujao mwaka huu.
Hayo yamesema na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele wakati akitembelea vituo mbalimbali vya uboreshaji wa Daftari hilo Katika halsmahauri za Mkoa wa Ruvuma.
“Nawasihi wananchi wa mikoa 15 ambayo awamu ya pili ya Uboreshaji Daftari inafanyika wandelee kujitokeza kuja kuboresha, waendelee kujiandikisha lakini pia kuwaondoa wale ambao hawastahili kuwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, tumebakiwa na siku chache zinazotakiwa kuendelea na zoezi,” amesema Jaji Mwambegele.

Jaji Mwambegele amesema zoezi la uboreshaji wa wa awamu ya pili linakwenda sambamba na uwekaji wazi wa Daftari la awali la kudumu la wapiga Kura ambalo linatoa fursa kwa wananchi kukagua, kufanya marekebisho ya taarifa za wapiga kura.
Pia, uwekaji wa pingamizi dhidi ya wapiga kura waliomo kwenye daftari ambao hawana sifa na litabandikwa katika vituo vyote vilivyotumika wakati wa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya kwanza.
Akizungumzia kuhusu mwenendo wa zoezi hilo kwa ujumla Jaji Mwambegele amesema zoezi linakwenda vizuri na mwitikio wa wananchi ni mzuri kwani maeneo aliyotembelea katika mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma wananchi wamejitokeza vituoni kujiandikisha, kuboresha taarifa zao pamoja na kutoa taarifa za watu waliopoteza sifa za kuwepo kwenye Daftari hilo.
“Kwa ujumla wake zoezi linakwenda vizuri na wananchi wengi wamejitokeza kwaajili ya kuboresha taarifa zao, wamejitokeza pia kwaajili ya kuboresha taarifa zao.
“Wale ambao hawastahili kuwepo katika Daftari la Kudumu la Wapiga kura wamefutwa,katika kila kituo nilichokwenda wameniambia kuhusu wale walio waandikisha, waboresha na wale waliowafuta,” amesema.
Uboreshaji wa Daftari unafanyika kwa mizunguko mitatu ambapo mzunguko wa kwanza unajumuisha mikoa 15, mzunguko wa pili utajumuisha mikoa 16 na mzunguko wa tatu utajumuisha vituo vya magereza na vyuo vya mafunzo.

Mikoa inayohusika kwenye mzunguko wa kwanza wa uboreshaji ni pamoja na Iringa, Geita, Kagera, Mara, Shinyanga, Mwanza, Simiyu, Rukwa, Tabora, Katavi, Kigoma, Ruvuma, Mbeya, Njombe na Songwe ambapo zoezi hilo lilianza kutekelezwa tangu Mei 1 na linataraji kukamilika Mei 7 mwaka huu.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti Maafisa Waandikishaji kutoka Majimbo ya Nyasa, Khalid Khalifa na yule wa Jimbo la Mbinga Mjini, Amina Hamisi Seif wamesema zoezi la Uboreshaji katika maeneo yao linakwenda vizuri na kuwahimiza wananchi kuendelea kujitokeza.
“Kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa tumekwisha andikisha wapiga kura wapya 436 na kuboresha taarifa za wapiga kura 415 wakati wapiga kura 68 wamepoteza sifa na kufutwa katika Daftari la Kudumu, bado tuzazo siku hivyo niombe kutumia fursa hii kuwataka wananchi waendelee kujitokeza,” amesema Khalifa.
Katika awamu ya pili ya uboreshaji, wapiga kura wapya 1,396,609 wataandikishwa, wapiga kura 1,092,383 wataboresha taarifa zao na wapiga kura 148,624 watafutwa kwenye Daftari kwa kukosa sifa za kuendelea kuwepo kwenye Daftari,” amesema Jaji Mwambegele.
Tume iliboresha Daftari la Kudumu la Wapiga Kura awamu ya kwanza kuanzia tarehe 20 Julai, 2024 na kukamilisha tarehe 25 Machi, 2025.
More Stories
Balozi Kaganda ahimiza ushirikiano kwa watumishi wa ubalozi
Mbunge ahoji matumizi holela ya msumeno nyororo
PPRA,WEDAC,wawajengea uwezo wanawake wajasiriamali