October 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Hatua kali kuchukuliwa kwa vituo vya malezi ya watoto wadogo ambavyo havijasajiliwa

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

OFISI ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma imewataka wamiliki wa  vituo vyote vya kulea  watoto wadogo mchana na Makao ya watoto kusajili ndani ya miezi mitatu kuanzia sasa vinginevyo hatua kali zitachukuliwa kwa watakaokahidi ikiwemo kuvifunga vituo hivyo.

Hayo yamesemwa na Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Dodoma Josephine Mwaipopo wakati wa mafunzo ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (MMMAM) kwa  wamiliki wa shule binafsi zenye watoto wadogo na vituo vinavyolea watoto wadogo mchana na Makao ya Watoto katika mkoa wa Dodoma.

Amesema,lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha wahusika hao wanakuwa na uelewa wa pamoja katika kutoa huduma kwa kufuata mingozo ya serikali inayotokana na sheria ya mtoto Na.21 ya 2009 marejeo ya 2019 na muongozo wake wa uendeshaji na usimamizi wa Makao na vituo vya kulelea watoto wadogo wa 2012.

Miongozo inataka Makao na vituo hivyo lazima vitoe huduma kwa kufuata viwango ,kanuni na taratibu zilizowekwa na serikali ili kuhakikisha huduma bora na zenye viwango zinatolewa

“Kama tusipoweza kukaa pamoja na kila mmoja akawa na uelewa wake kwa namna moja ama nyingine hatuwezi kufika katika kuwalea watoto maana kila mmoja atakuwa anakimbia kivyake

“Serikali inatambua mchango na jitihada zinazotolewa na  vituo hivyo kwamba wadau hawa ni muhimu katika kuhakikisha malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya watoto pamoja na kuwasaidia watoto walio katika mazingira hatarishi kupata huduma kwa mujibu wa miongozo na sheria kwamba watoto hao wana haki ya kusoma,kucheza na kupata stahiki zote kama watoto wengine ili waweze kufikia ukuaji timilifu na wenye tija.,

 “Kwa Dodoma tulikuwa bado hatujaunganisha pamoja nguvu ya wadau kama hawa ambao wapo zaidi ya 200 ,hii italeta manufaa makubwa ,kwa hiyo kikao hiki kilikuwa kwa ajili ya kukaa pamoja kujua changamoto zao , kujua serikali inataka nini ,kujua changamoto zao na namna ya kuzitatua ,lakini pia kupeana wajibu katika kuwahudumia watoto pasipo kukiuka taratibu ,sheria na miongozo ya kulea watoto.

Kwa mujibu wa Mwaipopo kikoa hicho kimekuwa na mafanikio kwani kimeweza kufahamu kuwa zaidi ya asilimia 60 ya vituo vya kulea watoto wadogo mchana ,havijapata usajili.