October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

HAIPPA PLC,yainua jamii kiuchumi

Na Raphael Okello, Timesmajira Online,Musoma

Kampuni ya HAIPPA PLC,imewezesha jamii kuinuka kiuchumi kwa kufungua masoko na kukuza mtaji.Hivyo Mkuu wa Mkoa wa Mara Kanali Evance Mtambi ameipongeza kampuni hiyo kwa jitihada hizo.

Akisoma hotuba katika mkutano mkuu wa pili wa Wanahisa wa HAIPPA PLC,kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mara,Kanali Evance Mtambi,mwakilishi kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mhandisi Mwita Chacha, amesema kampuni hiyo ni ya umma, yenye sera nzuri ya ubunifu, masoko na ukuzaji wa mtaji.

Hivyo amewataka wananchi na wajasiriamali kuongeza hisa zao.Na ambao hawajanunua waende wakanunue hisa hizo.Pia wakazi wa Mkoa wa Mara wawekeza katika sekta ya mifugo, kilimo, uvuvi , utalii , madini na uhifadhi.

Awali Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa HAIPPA PLC Bonface Ndengo, amesema kampuni hiyo ilianzishwa mwaka 2022 ikiwa na wawekezaji nane ambao walinunua hisa 3400.

Kwa mujibu wa Ndengo, amesema wameanzisha kampuni tanzu mbili , ya kwanza ni HAIPPA Microfinance kwa ajili ya kutatua changamoto za mitaji kwa wakulima, wajasiriamali wadogo na wahitimu wanaotoka kwenye mifumo ya elimu.

Amesema kampuni ya pili ni BIG4 LIMITED, ambayo ni kampuni ya teknolojia na uhandisi, inayojengwa ili kuzifikia fursa za kibiashara kwenye sekta ya madini, nishati, ujenzi, kilimo na miundombinu.

Mwenyekiti wa Bodi ya HAIPPA PLC, Dkt. Bonamax Mbasa ameeleza kuwa kampuni hiyo,ndiyo suluhisho pekee la tatizo la mtaji kwa wajasiriamali wadogo.

Amesema ifikapo Desemba mwaka huu HAIPPA PLC itakuwa na maonesho jijini Mwanza ambayo yatashirikisha kampuni kubwa za kimataifa kutoka mataifa mbalimbali.