March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

EWURA yasisitiza umuhimu  wa kuzingatia mikataba ya huduma kwa wateja

*Yatumia wiki ya huduma kwa wateja kutoa elimu kwa wananchi

*Wananchi zaidi ya 200 watembelea banda la EWURA

Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza 

Mamlaka za maji pamoja na TANESCO,zimetakiwa kuzingatia mikataba ya huduma kwa wateja pamoja na maadili ya utumishi wa umma kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora.

Hii ikiwa ni pamoja na kuzingatia katazo  la kutowakatia wananchi maji siku za mwisho wa wiki(weekend days) pamoja na sikukuu.

Hayo yameelezwa Oktoba 10,2025 na Meneja wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji(EWURA),Kanda ya Ziwa, George Mhina,katika Wiki ya Huduma kwa Wateja duniani kwenye banda walioweka chini ya jengo la PSSSF  ambalo ndipo ofisi za mamlaka hiyo  Kanda hiyo zilizopo jijini Mwanza,ambapo wametumia wiki hiyo kutoa elimu kwa wananchi.

Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa, George Mhina, akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani atika banda la mamlaka hiyo eneo la jengo la PSSSF, katika Wiki ya Huduma kwa Wateja

Mhina amesema,kupitia sheria ya maji,umeme na EWURA,mamlaka hiyo imepewa mamlaka ya kusimamia mikataba ya huduma kwa wateja.

Kwamba kila mamlaka zote za maji pamoja na TANESCO,zinatakiwa kuwa na mkataba wa huduma kwa wateja,ambao unaelezea haki na wajibu wa mtoa huduma na mteja.

“Lakini kupitia sheria zetu utaona kuna vitu vingi ambavyo baadhi za mamlaka za maji na Tanesco hawazitekelezi, mfano tukizungumzia kumkatia mteja maji,Sheria pamoja na mkataba wa huduma kwa wateja,ina kataza mteja asikatiwe huduma siku za mwishoni mwa wiki(weekend) na siku za sikukuu ni marufuku,”amesema Mhina.

Mhina amesema,pia Sheria na mkataba wa huduma kwa wateja,inamtaka  mtoa huduma aidha ni  mamlaka ya maji au TANESCO,kunapokuwa na tatizo la huduma itakayoathiri idadi kubwa ya watu pengine ni mtaa au Wilaya,kwa zaidi ya saa sita basi anatakiwa awataarifu wateja wake.

Pia kuna makatazo mengine na wajibu ambao mamlaka hizi zinatakiwa kufanya mfano kumfungia mteja huduma ndani ya siku saba au siku 30 baada ya kuwa amefanya malipo.

“Lakini kinachotokea kwa masikitiko hata kupitia wiki hii ya huduma kwa wateja kwa orodha ya waliotutembelea katika banda letu ni zaidi ya 200,kati yao malalamiko mengi yameangukia kwenye upande wa huduma ya maji ikiwa ni zaidi ya asilimia 92,”amesema Mhina na kuongeza:

“Wengine wanasema wamelipia huduma lakini hawajaunganishwa kwa zaidi ya miezi mitatu huku wengine wamekatiwa huduma bila kupewa notisi.Pia tunajua kuna maeneo hapa Mwanza yanachangamoto ya maji,yanaweza yasitoke hata siku mbili au tatu,lakini mamlaka husika haziwajibiki na hazitoi notisi kwa wateja wao,”amesema.

Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa, George Mhina, akifafanua jambo kwa mmoja wa wananchi wa Jiji la Mwanza alietembelea banda la mamlaka hiyo eneo la jengo la PSSSF, katika Wiki ya Huduma kwa Wateja

Hata hivyo Mhina, amesisitiza kuwa kama wasimamizi,wanachukua jambo hilo kwa umakini na kuhakikisha mamlaka hizo kwanza zinatangaza kwa wateja wao mikataba ya huduma kwa wateja ili wananchi waweze kujua haki zao na kufahamu wajibu wao.

“Lakini pia tutapita kwa wananchi kuwaelezea hiyo mikataba ya huduma kwa wateja walionayo hawa watoa huduma wetu,ili wananchi wanapokosa huduma  wajue wanachukua hatua gani ikiwa ni pamoja na kuwasilisha malalamiko EWURA kwa kigezo cha mamlaka husika imeshindwa kuzingatia na kutekeleza mkataba wake,”amesema Mhina.

Ofisa Mwandamizi wa Huduma kwa Wateja wa EWURA Jessica Sewando(kushoto) akizungumza na mteja aliyefika katika banda la mamlaka hiyo katika wiki ya huduma kwa wateja