September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Elezeni mtakavyoshughulikia masuala ya watoto’

Na Suleiman Abeid,TimesMajira Online. Shinyanga

VYAMA vya Siasa katika Jimbo la Shinyanga Mjini vilivyosimamisha wagombea kwenye nafasi za udiwani na ubunge vimeshauriwa pia kuelezea katika mikutano yao ya kampeni ni jinsi gani watakavyoshughulikia masuala ya watoto iwapo watapewa ridhaa ya kuwaongoza wananchi.

Ushauri huo umetolewa mwishoni mwa wiki na baadhi ya wakazi wa Shinyanga, waliohojiwa kwa nyakati na maeneo tofauti ambapo walisema pamoja na wagombea kunadi sera na ilani zao za uchaguzi, lakini hawazungumzii kwa kina masuala yanayohusu haki za watoto.

Wananchi hao wamesema mara nyingi wagombea wamekuwa wakizungumzia masuala ya jumla yanayohusu jamii wakielezea ni jinsi gani watakavyoyashughulikia iwapo watachaguliwa katika nafasi wanazogombea mfano ujenzi wa barabara, maji na masuala ya afya bila kugusa mambo yanayohusu haki za watoto.

Baadhi ya watoto waliokutwa kwenye mikutano ya kampeni za wagombea ubunge katika Jimbo la Shinyanga mjini kwa tiketi ya Chama cha ACT – Wazalendo na CCM walikiri kutosikia hoja yoyote inayozungumzia masuala ya watoto kwa undani mbali ya ahadi za kuboreshwa kwa elimu.

“Mimi ninasoma darasa la sita, mara nyingi napenda kuwasikiliza wagombea wakijinadi kwenye mikutano yao ya kampeni, ukweli sikumbuki kama kuna mgombea anayezungumzia kwa kina masuala yanayotuhusu, sanasana wanachozungumzia ni kuboresha elimu,” amesema Sostenes Boniface mkazi wa Ibinzamata.