April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt. Magufuli kuanza na vitakavyokuza uchumi

Na Penina Malundo,TimesMajira Online, Simiyu

MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) ambaye pia ni Mwenyekiti wa wa Chama hicho, Dkt. John Magufuli amesema ili kuwa na uchumi imara katika nchi ni lazima uanze na vitu vinavyochochea uchumi huo.

Dkt. Magufuli amesema hayo leo Mkoani Simiyu wakati akihutubia mkutano wa kampeni za kuomba kura kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 28 mwaka huu.

Amesema, katika nchi yoyote ukitaka kujenga uchumi ni lazima uanze na vitu vinavyochochea uchumi ikiwemo miundombinu ya maji, barabara, ndege pamoja na nishati kwani hauwezi kujenga uchumi ikiwa vitu vinavyochochea uchumi havijaendelezwa.

“Hata Mungu alipotaka kuiumba dunia hakuanza na watu, alianza na ardhi ili watu waje waitumie kulima na binadamu watakapokwenda katika ardhi alitaka wakaitawale na alitumia siku sita na ya saba akampumzika,”amesema na kuongeza.

“Nilipoingia madarakani nilitumia mbinu ya kujenga uchumi wa kisasa katika nchi hii na ndio maana tulianza na miundombinu. Nakumbuka Bariadi watu walikuwa wanakufa bila kutibiwa hospitali na walikuwa wanabebwa kwenye tela za Ng’ombe,”.

Mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. John Magufuli akiongea na wananchi wa Mkoa wa Simuyu katika viwanja cya Shule ya msingi Somanga

Pia amewaahidi wananchi wa Simiyu kuwa endapo wakimchagua tena miaka mitano ijayo atahakikisha ndani ya miaka mitatu ya utendaji wake atahakikisha anamalizia uwekaji wa umeme katika vijiji vilivyobaki.

Amesema, jumla ya Sh. bilioni 206.2 zimetekeleza mradi wa ujenzi wa barabara za lami na barabara za changarawe wakati katika nishati zimetumika Sh. bilioni 81.1 kutekeleza miradi ya umeme na kufikia vijiji 209 katika mkoa huo huku ujenzi wa kituo cha kupoza umeme ukigharimu kiasi cha Sh. bilioni 75.

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana, Henry James amesema, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli ilibeba maono na dhamira ya kutengeneza mazingira ya kuwezesha vijana nchini kuwa huru kufanya shughuli zao bila kusumbuliwa.

Amesema, pia amekuwa karibu na vijana kwani wamekuwa wakijishughulisha na ujasiriamali kila mahali bila tatizo lolote