Hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya yakabidhiwa mashine mbili na Daktari bingwa wa watoto
Na Esther Macha,TimesmajiraOnline,Mbeya
DAKTARI Bingwa wa watoto Dkt.Angela Leonard amekabidhi Mashine mbili za kutoa dawa za mfumo wa kupumua kwa watoto wanaokabiliwa na magonjwa hayo(nebulizer mashines) kwa hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya ikiwa ni sehemu ya shukrani zake kwa hospitali hiyo pamoja na watumishi kwa ushirikiano waliompatia kipindi cha utekelezaji wa majukumu yake akiwa Katika hospitali hiyo .
Akikabidhi msaada huo kwa mkurugenzi mtendaji wa hospitali ya Rufaa kanda ya Mbeya leo Februari 11,2025 ameeleza kuwa wameamua kutoa msaada huo ili kuonyesha moyo wa shukrani kwa jamii aliyoishi nayo na kuihudumia vievile kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha sekta ya afya nchini.
![](https://timesmajira.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/img-20250211-wa02615192568055165376274-1024x683.jpg)
“Naamini kuwa, kila mtoto ana haki ya kupata matibabu bora,ninatumaini kuwa mashine hizi zitarahisisha mchakato wa matibabu na kuokoa maisha ya watoto wengi, pia nikiwa sehemu ya jamii naunga mkono jitihada za Serikali yangu katika juhudi za kusaidia upatikanaji wa huduma bora za afya ya mama na mtoto nchini.” Amesisitiza Dkt. Angela
Hata hivyo amesema kwamba eneo la watoto ni muhimu hivyo ndiyo Sababu ya kutoa mashine hizo mbili kwa hospitali yetu ya Rufaa kanda ya Mbeya ili kuhudumia watoto ambao wanakua ikiwa na mfumo wa kupumua.
Akizungumza wakati wa kupokea vifaa hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya Dkt. Godlove Mbwanji, amemshukuru Dkt. Angela kwa mchango huo mkubwa ambao utasaidia watoto wanaokabiliwa na magonjwa ya mfumo wa kupumua.
Dkt.Mbwanji amesema,“Mashine hizi ni muhimu sana katika hospitali yetu kwani zitatumika katika kutoa huduma bora za matibabu kwa Watoto hasa wanaosumbuliwa na magonjwa kama asthma, pneumonia na magonjwa mengine ya upumuaji.”
Aidha Dkt.Mbwanji, ametoa rai kwa jamii na taasisi mbalimbali kuwa na tabia ya kutoa sehemu ya shukrani zao za baraka ya mafanikio wanayoyapa kwa kupeleka misaada ya rasilimali fedha na vifaa tiba kwenye hospitali ili kusaidia wananchi,kwani jukumu la kuboresha upatikanaji wa huduma za afya nchini ni la kila mmoja wetu.
Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya inatoa huduma za matibabu kwa wakazi wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, hivyo msaada huu ni hatua muhimu katika kuboresha huduma zinazotolewa.
![](https://timesmajira.co.tz/wp-content/uploads/2025/02/img-20250211-wa02623844905882483542392-1024x683.jpg)
More Stories
Wasira:Uchaguzi Mkuu utafanyika wanaCCM,Wananchi jiandaeni
Rais Dkt.Mwinyi atuma wajumbe kujifunza utekelezaji wa PJT-MMMAM
Katavi yazindua mkakati wa kupambana na udumavu