October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dk. Mpango amwakilisha Samia sherehe za Uhuru wa Lesotho

Na Mwandishi Wetu, Timesmajiraonline, Lesotho

MAKAMU wa Rais Dkt. Philip Mpango ameshiriki katika sherehe za Miaka 58 ya Uhuru wa Lesotho na Miaka 200 ya kuanzishwa kwa Ufalme wa Lesotho zilizofanyika katika Uwanja wa Setsoto Mjini Maseru.

Makamu wa Rais amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sherehe hizo zilizohudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Wakuu wa Nchi na Serikali pamoja na washirika wa maendeleo wa Taifa hilo wa ndani na nje ya Bara la Afrika.

Awali Makamu wa Rais alikutana na kufanya mazungumzo na Mfalme wa Lesotho Mfalme Letsie III katika Ikulu ya Kifalme iliyopo Maseru nchini humo. Mazungumzo hayo yamelenga kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Lesotho.

Makamu wa Rais aliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mashoeshoe Mjini Maseru na kupokelewa na na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi wa Lesotho Mhe.Neo Matjato Moteane.

Makamu wa Rais ameambatana na Waziri wa Nchi Afisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Harusi Said Suleiman, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dennis Londo pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini Mhe. Balozi James Bwana.