April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC Ilemela aanza kutoa maagizo kwa watendaji

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online,Mwanza

MKUU wa Wilaya ya Ilemela Hassan Masalla,amemtaka Mtendaji wa Kata ya Buswelu,kuwapanga watendaji wake pamoja na kukaa na wenyeviti wake wa mitaa,ili waanze kutatua changamoto ambazo zimetajwa na wananchi wa kata hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Hassan Masalla, akizungumza na wananchi wa Kata ya Buswelu,ikiwa ni mwanzo wa ziara yake ya awamu ya pili ya kata kwa kata wilayani humo ya kukagua utekelezaji wa shughuli za maendeleo, kuhamasisha wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya UVIKO-19, kusikiliza keri na changamoto za wananchi na kisha kuzipatia ufumbuzi,uliofanyika shule ya msingi Buswelu.(picha na Judith Ferdinand)

Akizungumza wakati mkutano na wananchi wa Kata ya Buswelu ikiwa ni mwanzo wa ziara yake ya awamu ya pili ya kata kwa kata wilayani humo ya kukagua utekelezaji wa shughuli za maendeleo, kuhamasisha wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya UVIKO-19,kusikiliza kero na changamoto za wananchi na kisha kuzipatia ufumbuzi,uliofanyika uwanja wa shule ya msingi Buswelu.

Masalla,amesema,katika kutatua changamoto za wananchi,wanao wenyeviti wa mitaa,watendaji wa mitaa na kata,hivyo lazima wawatumie kwa sababu wanalipwa mishahara na serikali na kuwataka watendaji kusimama kwenye mstari.

“Kila Mtendaji wa kata hiyo,akae na watendaji wake na wenyeviti wa mitaa yake watatue changamoto ambazo wananchi wamezitataja kwani nyingi zipo ndani ya uwezo wao,’ amesema.

Amesema kuwa endapo watafanya mikutano na wananchi anaamini kuwa changamoto nyingi zitatauliwa na hata pia hakutakuwa na malalamiko kwa diwani,Mkuu wa Wilaya,Mbunge wala Mkurugenzi.

“Dhima ya serikali na kazi iliotuweka hapa ndio hii, kwa hiyo kaa, wapange watendaji wako,kaa na wenyeviti wako anzeni kutatua changamoto ambazo zimetajwa hapa,kwa sababu nyingi zipo kwenye uwezo wenu,zile ambazo zimeshindikana tuwe na kazi ya kuwasiliana kwa Mkurugenzi cheza na ofisi yangu,kwa Mkurugenzi kukilegalega mimi wajibu wangu ni kumkumbusha Mkurugenzi nini cha kufanya,”amesema Masalla.

Pia amesema,kuna maeneo Mtendaji akitekeleza hawataingilia na atakaposikia wananchi wametoa faini kwa sababu ya uchafu atafurahia kwa kuwa kiongozi atakuwa amesimama kwenye mstari.

“Kikubwa atende haki,asimamie haki na kufuata utaratibu,watu lazima wawe na nidhamu wasimame kwenye mstari huku akisema serikali imeanzia kule chini mtaani,’ amesema.

Hivyo amewataka wenyeviti wafanye kazi kwani wana sheria wamepewa,wazitumie hizo sheria na kuna kutoza faini,watoze hizo faini kwa sababu kuna watu watakuwa wameshindwa kutimiza maagizo.

“Tunaangalia Wilaya nzima hatuwezi kuangalia eneo moja hivyo ni wajibu wa kila mmoja kukaa kwenye mstari na kutimiza sehemu ya wajibu wake,wenyeviti nimewaambia waliomba nafasi hizo kwa sababu walijipima na walijua wanao uwezo wa kufuatilia matatizo ya wananchi,wajibu wao wakasimamie vitu kwa sababu vipo ndani ya mamlaka zao,”.

Sanjari na hayo,amesema,amekuja Ilemela kufanya kazi na siyo vinginevyo,hivyo atafanya kazi kwa kadri yake na taratibu zinavyowataka wafanye.

“Niwaombe tu tushirikiane wote,yote mliokuja kusema hapa,mmezungumza kwa uchungu, mmezungumza vizuri lakini na nyinyi bado ni sehemu ya kutatua haya,sisi tupo hapa ndani ya masaa mawili,tutaondoka,tutawaacha ninyi huku nyuma,nisinge tamani nije hapa baada ya miezi mitatu niitishe tena mkutano tuje tuzungumze stori zinazofanana na haya tuliozungumza hapa, vinginevyo yawe nje ya uwezo wetu,”amesema Masalla.

Kwa upande wao baadhi ya wananchi wa kata hiyo,walimuomba Mkuu wa Wilaya hiyo kuwasaidia changamoto mbalimbali zinazokabili ikiwemo kero ya daladala kukatisha ruti.