April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti Mtendaji wa MYCN Brightus Titus, akizungumza katika moja ya mafunzo kwa vijana kwa ajili ya kujiinua kiuchumi,kupitia mradi wa vijana na Mkwanja.

Corona yaathiri utendajikazi wa shirika la MYCN

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online,Mwanza

SHIRIKA la Mtandao wa Vijana na watoto Mwanza(MYCN),limesema katika kutekeleza mradi wa Vijana na Mkwanja mwaka 2020 katika Manispaa ya Ilemela zipo sababu mbalimbali ikiwemo ya Covid-19,iliosababisha utekelezaji wake kuchukua muda mrefu zaidi.

Akizungumza na Majira ofisini kwake,
Mwenyekiti Mtendaji wa MYCN Brightus Titus,amesema mradi huo ulikuwa umejikita katika kuhakikisha vijana wanajikomboa kiuchumi ulitekelezwa katika kata za Buswelu,Nyasaka, Ilemela, Shibula,Kitangiri na Nyamanoro,zilizopo Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Baadhi ya vijana ambao walipatiwa mafunzo ya kujikwamua kiuchumi kupitia mradi wa Vijana na Mkwanja wa MYCN.

Lakini kutoka na wimbi la kwanza la mlipuko wa ugonjwa wa Corona, ilileta ugumu katika utekelezaji wa mradi huo hivyo kuna muda walisitisha shughuli za mradi.

Na kusababisha kuongeza muda zaidi ya utekelezaji wa mradi huo kwani ulianza mwaka 2019 na uritarajiwa kukamilika 2020 lakini kutokana na corona ulikamilika Machi mwaka huu.

Titus amesema,katika utekelezaji wa mradi huo walikutana na changamoto ya kushindwa kuwafikia vijana kwa wakati kutokana na mlipuko wa COVID-19 mwaka jana.

Amesema iliathiri mfumo wa utendaji kazi kwenye mradi huo,maana awali walikuwa wanawafikia vijana moja kwa moja na kwenye makundi,na kuweza kujadili juu ya changamoto zao na kuweza kukutana na maofisa na viongozi wa Serikali ili kuweka mikakati ya kuzitatua changamoto hizo.

Lakini baada ya corona COVID-19 kuingia nchini mfumo ulibidi kubadilika kidogo kwa sababu ilikuwa hairuhusiwi misongamano ya watu,ilibidi kubadilisha mfumo huo na kuanza kutumia vyombo vya habari.

Pia amesema,katika matumizi ya vyombo vya habari changamoto ni kuwa msikilizaji au mtu anayesoma ile habari,ambaye mradi ndio umemlenga unakuwa hauna uhakika kama kile kitu alicho kisikia au kukisoma anaenda kukifanyia kazi.

“Ilikuwa ngumu kumfuatilia kuwa huyu mtu fulani umesikiliza kipindi na umechukua hatua gani,umeenda serikali za mitaa umemkuta Ofisa Maendeleo amekuelekeza namna ya kuanzisha kikundi au amekuelekeza jinsi gani unaweza kuomba mkopo,”ameeleza.

Aidha amesema,hali hiyo pia iliondoa ule ukaribu wa mtu kuonana ana kwa ana na pia walipunguza ziara za kukutana na vikundi moja kwa moja kwaio ikabidi kuanza kukutana na mtu mmoja mmoja kitu ambacho ni gharama,maana kufikia vijana 184 katika maeneo yao ya uzalishaji inakuwa ni changamoto sana kwa sababu za kibajeti ambapo hawakuwa na fungu kulingana na mradi ulivyokuwa.

“Kutokana na kushindwa kuwafikia vijana moja kwa moja kumesababisha baadhi ya vikundi vingine kudorora kwa vile vimeisha zoea kusukumwa na vingine vilishindwa kwenda vizuri kutokana na vile tulivyokuwa tumefanya makadirio (projection) ya mradi haikuweza kwenda vile tulivyotarajia,”amesema

Ofisa Miradi wa MYCN Generosa Ladislaus,amesema, miongoni mwa changamoto zilizojitokeza wakati wa kutekeleza mradi huo ni pamoja na mlipuko wa virusi vya Corona(COVID-19) ambao umechangia kikwamisha ufikiwaji na uhusishwaji wa idadi kubwa ya vijana.

Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Hassan Masala akizungumza na Majira ofisni kwake Picha zote na Judith Ferdinand

Kwa upande wake mmoja wa vijana wa Kata ya Nyamanoro Denis Bashaija, amesema katika mlipuko wa kwanza wa COVID-19,wapo baadhi ya vijana walijikuta wanashindwa wafanye nini hususani wale ambao walikuwa hawana ujuzi au mafunzo ya kujikwamua kiuchumi.

Hivyo kujikuta wakikaa tu mtaani na muda mwingi wakitumia katika mitandao ya kijamii,kuangalia tamthilia, kushindwa kufanya shughuli za kiuchumi kutokana na wadau wengi pamoja na serikali katika kipindi hicho kujikita zaidi katika kujikinga na kupambana na corona.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Hassan Masala,akizungumza na Majira ofisini kwake amesema,kama wilaya mkakati wao ni kuangalia makundi yale ambayo yana stahiki kupatiwa nguvu ya kufanya kazi yanapata kitu hicho kwa mujibu wa sheria na taratibu ambazo zipo katika nchi.

“Na sisi kama wilaya tuna vikundi ambavyo tayari tunatoa fedha za mikopo kwa vijana na hata kipindi cha mwenge miradi mingi tumezundua yenye lengo la kuweka vijana pamoja kuwapa elimu inayohusiana na mambo mbalimbali ikiwemo suala la athari za dawa za kulevya,magonjwa mbalimbali yanayoweza kusitisha ndoto zao,”amesema Masala.