September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Changamoto ya zahanati kisiwani Bezi yapatiwa ufumbuzi,milioni 206 zatengwa

Na Judith Ferdinand, Timesmajira Online,Mwanza

Katika kutatua kero ya muda mrefu ya ukosefu wa huduma za afya karibu kwa wananchi wa kisiwa cha Bezi kilichopo Kata ya Kayenze wilayani Ilemela mkoani hapa kiasi cha milioni 206 kimetengwa na serikali kwa ajili ya kusogeza huduma hiyo kisiwani humo.

Ambapo fedha hizo ambazo zitatumika kujenga zahanati pamoja na nyumba za watumishi kisiwani humo zimetengwa ,kupitia Mpango wa kunusuru Kaya masikini (TASAF-OPEC 4 ).

Akizungumza Julai 15,2024 wakati wa ziara yake Kata ya Kayenze mtaa wa Iponyabugali viwanja vya Nyamdoke yenye lengo la kusikiliza kero na kutoa mrejesho wa vikao vya Bunge kwa wananchi Mbunge wa Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula amesema changamoto ya wazazi kujifungulia njiani wakati wa kufuata huduma za afya, umbali mrefu na gharama kubwa imepata utatuzi baada ya serikali kuweka mpango wa kuboresha huduma za afya katika eneo hilo.

”Serikali imetenga fedha kwa ajili ya nyumba za watumishi mbili kwa milioni 103 na zahanati milioni 103, Kikubwa tuendelee kumuombea na kumuunga mkono Rais,”amesema Dkt.Angeline.

Pia amewataka wananchi wa Kata hiyo kusimamia na kulinda vifaa vya ujenzi wa miundombinu hiyo visiibiwe ili kukamilisha miradi mbalimbali inayotekelezwa pamoja na kuwaripoti wabadhirifu wote wa mali za umma watakaojitokeza ili Sheria ichukue mkondo wake

Gabriel Remmy ni Msanifu Majenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela amefafanua kuwa mradi huo wa zahanati utakuwa na idara mbili za RCH na OPD pamoja na nyumba moja itakayojumuisha watumishi wawili huku akiongeza kuwa kinachosubiriwa ni mifumo ya malipo kuanza kufanya kazi ili mradi uweze kutekelezwa.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Kayenze Issa Dida amewata wananchi wa Kata hiyo kuchangia na kushiriki shughuli za maendeleo ili jamii yao iweze kusonga mbele.

Joachim Sylvester ni mwananchi wa mtaa wa Iponyabugali kata ya Kayenze ambapo amempongeza mbunge Dkt Angeline Mabula kwa kufanya ziara katika mtaa wao kusikiliza kero na kuzipatia ufumbuzi.