July 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yaridhishwa utekelezaji Ilani

Na Daud Magesa, TimesMajira Online, Sengerema

KAMATI ya Siasa Mkoa wa Mwanza,imeridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo wilayani Sengerema yenye zaidi ya bilioni 20 ukiwemo wa maji wa Nyasigu-Lubungo-Ngoma utakaogharimu kiasi cha bilioni 13.7 na kuwahudumia wananchi 52,800.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza, Michael Masanja ‘Smart’ akizungumza baada ya kamati hiyo kukagua tanki la maji la mradi wa Nyasigu-Lubungo-Ngoma,amesema kwa hatua ulipofikia umetekelezwa kulingana na fedha zilizotolewa.

Smart amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,Said Mtanda kufuatilia malipo ya mkandarasi ya kiasi cha bilioni 2.1 ili aukamilishe kwa mujibu wa mkataba,mradi huo ukikamilika ni mtaji kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa.

“Mkandarasi hana tatizo, kulingana na fedha aliyolipwa amefanya kazi kubwa ispokuwa changamoto ni hali ya malipo kuchelewa.Mkuu wa Mkoa mwaka huu tuna jambo letu,ukikamilika wananchi wataona tuliyofanya hivyo fuatilia hizo bilioni mbili alipwe haraka mradi ukamilike,”ameagiza.

Awali Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Sengerema (SEUWASA), Mhandisi Sadala Hamis amesema mradi huo unaotekelezwa kwa sh. bilioni 13.7 umefikia asilimia 36 na ukikamilika utanufaisha wananchi 52,800 wa vijiji saba vya kata za Igalula na Ngoma, wilayani humo.

Amesema mradi huo wa Nyasigu-Lubungo-Ngoma unatekelezwa na kampuni ya GEMEN hadi sasa amelipwa bilioni 1.7 na mradi unatakiwa kukamilike Desemba mwaka huu baada ya kuongezewa muda kutokana na changamoto ya malipo kuchelewa na mvua zilizokuwa zikinyesha na kusababisha usimame.

“Hadi Machi mwaka huu,mkandarasi amewasilisha hati ya malipo ya sh.bilioi 2.1 pia,changammoto ya mvua,anafanya kazi katika mazingira magumu na hivyo mradi umesimama,”amesema Mhandisi Hamis.

Aidha Kamati hiyo ya Siasa ya Mkoa wa Mwanza,ilikagua mradi wa daraja la Bulakala-Ngoma lililojengwa kwa milioni 640.8, kwa mujibu wa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza, Mhnadisi Ambrose Pascal, daraja hilo limekamilika kwa asilimia 100.

Kwa niaba ya Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Mwanza, Smart amesema,“Pia lilitakuwa kiungo kati ya Igalula na Sengerema mjini na litachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa Wilaya ya Sengerema,”.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Sengerema, Mark Makoye na Mkuu wa Wilaya hiyo,Senyi Ngaga kwa nyakati tofauti wamesema daraja hilo lilikuwa tishio wakati wa mvua lilisababisha vifo vya baadhi ya wananchi na mafuriko.

“Ni jambo la kupongeza serikali kwa kuridhia kutoa fedha ambapo limetekelezwa kwa wakati na mkandarasi mzawa,hivyo ni kipimo cha kuwaamini wakandarasi wa ndani,”amesema Makoye.

“Wananchi wengi walipoteza maisha kwa kusombwa na maji kupitia daraja hili,mwaka huu licha ya mvua kunyesha hatujapata taarifa ya kifo cha mwananchi yeyote, hivyo tunaipongeza serikali kwa kuondoa changamoto hiyo,”amesema Ngaga.