September 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM kuwaboreshea mazingira ya ufanyaji kazi wadau Mererani

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online,Manyara

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimepanga kuboresha mazingira mazuri katika eneo la Mererani, Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, ili kuwarahisishia mazingira bora ya ufanyaji kazi wadau wa maenendelo wa maeneo hayo.

Kauli hiyo imetolewa leo na Katibu wa NEC,Itikadi,Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa,CPA Amos Makalla, alipokutana na viongozi wa Chama ngazi ya Wilaya na wadau wa maendeleo wa Mererani na kusema kuwa,kuboreshwa kwa mazingira kutasaidia kuleta ajira na kuongeza uchumi wa Taifa.

“Changamoto za Mererani tunatambua ni nyingi mno na zitatatuliwa ikiwa pamoja na kuwaboreshea mazingira mazuri ya ufanyajikazi kwani tukiwaboreshea nyinyi kutasaidia mfanye vizuri na nyie mtoe ajira kwa wengine lakini pia kukuza uchumi wa nchi yetu”, amesema Makalla.

Pia, amewaomba wadau hao kuendelea kuipa ushirikiano CCM na Serikali hususani katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa, huku akiwasisitizia kuwa, CCM ndiyo chama chenye dhamana na kinachoweza kuwaletea maendeleo wananchi.

Aidha, wakati huo huo CPA, Makalla, amepata nafasi ya kuwatunuku vyeti vya mafunzo kwa wadau wa maendeleo na kusema kuwa CCM inatambua mchango wao na vyeti hivyo havina thamani kulingana na Maendeleo yanayofanywa na wadau hao Mererani.