September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CBT yawaonya viongozi, watendaji wa AMCOS

Na Ahmad Mmow,TimesMajira Online. Lindi

WAKATI wa uuzaji na ununuzi wa korosho ghafi kwa msimu wa 2020\21, ukitarajiwa kuanza mwanzoni mwa Oktoba mwaka huu Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) imetoa angalizo kwa wakulima, Vyama vya Msingi vya Ushirika (AMCOS) na wasafirishaji wawe makini ili kuepuka usumbufu utakaotokana kutozingitia ubora wa zao hilo.

Angalizo hilo limetolewa jana mjini hapa na Ofisa Ubora wa Korosho wa CBT, Joseph Merere wakati wa mafunzo ya siku moja ya udhibiti ubora wa korosho ghafi ngazi ya wakulima, ambayo ilitolewa kwa watendaji na viongozi wa AMCOS zilizopo wilayani Lindi.

Merere amesema ili kulinda ubora wa korosho na kuwezesha ili zipate soko zuri na wakulima wauze kwa bei zenye tija, kuna umuhimu na kila sababu ya wakulima, viongozi na watendaji wa AMCOS na wasafirishaji wazingatie ubora. Lakini pia wataepuka matatizo yanayoweza kuwakuta kutokana na kutozingatia ubora wa zao hilo.

Amesema wakulima watakaopeleka maghalani korosho chafu ikiwamo zisizokauka vizuri, watawajibika kwa gharama zitakazohitajika ili kuboresha korosho zao kwa viwango vinavyohitajika, lakini pia akionya kwamba wakulima watakaobainika kuweka vitu visivyokubalika, ili kuongeza uzito korosho zao watawajibika kwa mujibu wa sheria namba 18 ya mwaka 2009, kifungu cha 23(9).