May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Benki ya KCB yadhamini McEnroe Serengeti Cup 

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

KATIKA kuchochea kasi ya maendeleo na uwekezaji hapa nchini, Benki ya KCB imedhamini mashindano ya McEnroe Serengeti Cup yakiwa na lengo la kuutangaza utalii hapa nchini, kuptia mashindano hayo.

Mashindano hayo yanafanyika katika mbuga ya Serengeti, ambapo benki hiyo imewaleta magwiji wa mchezo wa tenis duniani, Patrick na John McEnroe kutoka nchini Marekani.

Mbali ya magwiji hao kushiriki mchezo huo, pia imewapa nafasi kujionea vivutio mbalimbali vya utalii Nchini, pamoja na kupata nafasi ya kutambua vipaji vya mchezo wa tenis jambo litakalo wafanya kuwa mabalozi wazuri wa Kimataifa Tanzania.

Akizungumza wakati wa mashindano hayo jana, Mkuu wa Masoko, Mawasiliano na Uhusiano wa Benki hiyo, Cristina Manyenye alisema KCB Benki ndio wadhamini wa mashindano hayo ambayo yanawahusisha wachezaji wakubwa wa mchezo wa tenis kucheza mchezo huo hapa nchini katika Mbuga ya Srengeti.

Alisema, katika kuhakikisha wanajivunia maliasili ya Tanzania, KCB Benki imeona ni muhimu sana na wao wakachangia katika hilo na wametoa dola za kimarekani 10,000 kwa ajili ya kuchangia mchezo huo ambao umefanyika katika mbuga hiyo ambayo maarufu hapa nchini.

“KCB Benki Tanzania, mbali na kuendeleza nia yetu ya kuibua fursa na kuinua utalii Nchini, tunaamini ziara hii itafungua milango ya uwekezaji pamoja na kuzinufaisha jamii za kitanzania kwa njia tofauti na kuchangia maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

“Tumeamua kufanya hivi sio kwa ajili ya mchezo tu bali  inakuza nchi yetu. Tunajua Serengeti imechaguliwa kama moja ya mbuga nzuri duniani, ukizingatia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan anakimbizana na suala la utalii hapa nchini, sisi kama Benki ya KBC tumeamua kumuunga mkono Rais wetu katika utalii huu.

“KCB Benki tupo hapa leo kwa ajili ya tukio hili ambalo tumelidhamini kwa dola za kimarekani 10,000 kiwango ambacho tunaamini kitayapa tija mashindano haya,” alisema Cristina.

Hata hivyo Cristina alisema, KCB Benki imeunga mkono mashindano hayo kwa asilimia kubwa ukizingatia wao ni Watanzania na benki hiyo imewekeza hapa nchini, kutokana na uchumi ulivyo wameaona hawana budi kuunga mkono juhudi za kuutangaza utali.

Alisema, Serengeti ni mbuga nzuri kwa hiyo wakiendelea kuitangaza itazidi kuvutia watalii na kutambulika zaidi duniani kwa hiyo wanajivunia sana kudhamini michezo hiyo.

Naye Mkuu wa biashara za rejareja na biashara ndogondogo na za kati kutoka benki hiyo, Abdu Juma alisema wao wapo Serengeti kwa ajili ya tukio kubwa ambalo ‘ameliita utalii wa kimichezo’ kwa mara ya kwanza limefanyika hapa nchini.

Alisema, katika mashindano hayo, kuna wachezaji mbalimbali maarufu dunia katika mchezo wa tenis ambao walishiriki lengo likiwa kuutangaza utalii wa Tanzania.

“Sisi kama KBC tumeingia hapa kwa sababu tunafanya biashara na watu ‘Tour Opereation’ ni wateja ambao tunawasapoti katika biashara zao na ndio hao waliondaa Tamasha kwa kushirikiana na serikali, kwa hiyo benki yetu tunawasaidia wateja wetu ambao wapo kwenye utalii.

“Lakini pia kuufanya utalii uzidi kwenda mbele zaidi, kama mnavyoona Rais wetu anavyozidi kuutanga utalii, hivyo na sisi hatuna budi kumuunga mkono kwani ni sekta muhimu sana kwa nchi yetu katika kuingiza kipato cha nchi kupitia utalii,” alisema Abdu Juma.