*Huku wagombea 69 ngazi ya Udiwani kupeperusha bendera ya vyama vyao
Na Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza
Jumla ya wagombea 16 kutoka vyama mbalimbali wameteuliwa kugombea nafasi ya Ubunge katika Jimbo la Ilemela mkoani Mwanza huku wagombea 69 wa ngazi ya Udiwani wakiteuliwa kushiriki katika kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kwa Kata 19, zilizopo jimboni humo.
Ambapo vyama 16 vya siasa ambavyo wagombea wake wameteuliwa ni CCK, DP, NLD, AAFP, SAU, MAKINI, UMD, N.R.A, ACT, UPDP, UDP, CUF, NCCR-MAGEUZI, ADC,CCM na CHAUMMA.
Akitoa taarifa Agosti 28, 2025, ofisini kwake,Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Ilemela,Herbert Bilia, amesema wagombea 17,walifanikiwa kuchukua fomu za uteuzi kwa ngazi ya Ubunge,kati yao 16 walifanikiwa kurejesha fomu hizo huku mmoja akishindwa kurejesha.
“Mmoja hakuteuliwa na hii imetokana na kuwa mgombea huyo kutoka chama cha ADA -TADEA hadi kufika saa 10 jioni Agosti 27, 2025 muda wa uteuzi hakuwa amerejesha fomu,hivyo kukosa sifa ya kuteuliwa,”amesema Bilia.
Bilia amesema,kwa upande wa ngazi ya Udiwani jumla ya wagombea 81 waliochukua fomu za uteuzi kati yao 69 walifanikiwa kurejesha fomu hizo na kuteuliwa kupeperusha bendera ya vyama vyao katika uchaguzi mkuu kwa nafasi hiyo huku wagombea 12 wakishindwa kuteuliwa kutokana na sababu kuu mbili.
Ametaja sababu hizo kuwa ni mgombea mmoja alikosa wadhamini huku wagombea 11 hawakuteuliwa kutokana na kutokurejesha fomu hadi muda wa uteuzi ulipofika ambao ni saa 10 jioni Agosti 27,2025.
Pia amesema,kwa mujibu wa kalenda ya uchaguzi mkuu wa Rais,Wabunge na Madiwani, Agosti 28,2025 kampeni zinaanza nchi nzima,hivyo amewahimiza wananchi kujitokeza katika kampeni hizo ili kusikiliza sera za wagombea na kuweza kufanya maamuzi sahihi.Huku akiwasihi wagombea kufanya kampeni kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni kama ilivyoelekezwa.
“Kwani uchaguzi ni nyenzo muhimu ya kutupatia viongozi wa kutusaidia kudumisha amani,utulivu na kutuletea maendeleo,”amesema Bilia.

More Stories
TAMWA yakumbusha jamii kupinga ukatili wa kijinsia kuelekea siku ta wanawake Duniani
Wanawake washauriwa kuchangamkia fursa za uchumi
Aida:Wanawake wakipata haki zote itapunguza migogoro