October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watahadharishwa kutoweka mamluki katika uchaguzi

Na Ashura Jumapili TimesMajira online Kagera,

Mkuu wa Mkoa wa Kagera,Fatma Mwassa amewatahadharisha wananchi wasiweke mamluki, wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba 27 mwaka huu,kwani kuwasababisha hatari kwenye nchi.

Hajath Mwassa, amesema hayo wakati akiongea na waandishi wa vyombo mbalimbali vya habari ofisini kwake,ambapo amedai kuwa Mkoa utachua hatua za kisheria kwa wahamiaji haramu ambao wameng’ang’ania kuishi mkoani humo,kama watajaribu kuhujumu uchaguzi wa serikali za mitaa kwa namna yoyote .

“Natambua kuna wahamiaji haramu wanaishi hapa kinyume cha sheria na wakati mwingine wanatumia rushwa ili kupata uongozi wakati wa kugombea, watakaobainika hatua kali zitachuliwa dhidi yao.Wahusika wa uchaguzi huo ni watanzania tu ,”amesema Hajath Mwassa.

Amesema wananchi wenye sifa wajitokeze kwenda kujiandikisha kwenye vituo vya uandikishaji wapiga kura,Mkoa umeandaa jumla ya vituo 3,833, ili wananchi wajitokeze kwa wingi kujiandikisha na wapate fursa ya kutumia haki yao ya msingi na kikatiba kupiga kura muda ukifika.

Amesema Mkoa wa Kagera unakadiriwa kuwa na watu wenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea ambao ni zaidi ya milioni 1.5 huku wanaume wakiwa zaidi ya laki 7.5 na wanawake zaidi ya laki 8.1.

Amesema uchaguzi utakuwa wa haki na huru, kwa wagombea wote watakaojitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi huo.

Sanjari na hayo amesema kampeni zitaanza Novemba 20 hadi Novemba 26 mwaka huu,na kuwataka wagombea wa vyama mbalimbali kufanya kampeni za kistarabu.