September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wasisitizwa kuchagua viongozi wanaohubiri amani

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

KUELEKEA Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Novemba 27, mwaka huu, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Juma Homera,amewahimiza wananchi kuchagua viongozi wanaohuburi amani na upendo katika Taifa.

Homera amesema hayo Septemba 26,2024 wakati wa ufunguzi wa mashindano ya ngoma za asili yajulikanayo kama Tulia Traditional Dance festival msimu wa nane, yanayofanyika uwanja wa ndege wa zamani Kata ya Iyela Jijini Mbeya.

“Chagueni viongozi ambao wataweza kulisaidia taifa hili kwa ajili ya maendeleo ya leo na kesho, lakini tuchague viongozi wanaohuburi amani na upendo,nimewakabidhi kazi Machifu,wahakikishe wanaliombea Taifa pamoja na viongozi wa dini,ili tupate viongozi bora na si bora viongozi,tusichague kwa mihemko ya watu,”amesema Homera.

Mkuu huyo wa Mkoa,amewahimiza vijana kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi ikiwemo serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.”Msiache kugombea ni muda wenu, msisubiri kesho, hakikisheni mnatumia nafasi hiyo katika maeneo yenu,”.

Homera amewaomba Madiwani wa Jiji la Mbeya, kupambana kuleta maendeleo kwa wananchi.Wakati uliobaki wakafanye mikutano ya hadhara,kuzungumza na wananchi,kusikiliza kero na kuzitatua.

Kwa upande wake, Chifu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Rocket Mwashinga, amesema kuwa walishapotea katika kuenzi mila na tamaduni, kwani kama mtu huna ngoma ya kwenu unakuwa umeshapotea na hujulikani ulipotoka.

Mwashinga amesema kwamba Mbunge wa Jimbo la Mbeya amekuwa na jitihada za kuongoza ngoma na kukumbusha wajibu vijana wa kuenzi utamaduni wao badala kusahau mila na desturi zao.

Mwenyekiti wa Machifu Tanzania, Antonia Sangalali,amewataka watanzania kutokubali kurubuniwa na watu,kwani amani ndo kila kitu na wapo hapo sababu ya amani .