September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia aahidi Mil. 500 Stars ikifuzu AFCON 2025

*Yaichapa Guinea 2-1

Na Mwandishi Wetu,Timesmajiraonline

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kutoa shilingi milioni 500, iwapo timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, itafuzu michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2025), itakayofanyika nchini Morocco.

Akitoa ahadi hiyo jana kwa niaba ya Rais, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma aliwatia moyo Taifa Stars huku akiwapa salamu kutoka kwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan iwapo watafuzu michuano hiyo.

“Tukifuzu kwenda AFCON 2025 ya Morocco kuna shilingi milioni 500 mezani,” alisema Mwinjuma akitoa salamu za Rais Samia kwenda kwa wachezaji wa Taifa Stars.

Taifa Stars ilifanikiwa kuondoka na alama tatu baada ya kuibuka na ushindi ugenini wa goli 2-1 katika mchezo wa pili wa kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON 2025, dhidi ya Guinea.

Mchezo huo wa Kundi H, ulichezwa jana kwenye dimba la Charles Konan Banny, Yamoussoukro nchini Ivory Coast, licha ya wenyeji kuonekana kuutawala mchezo.

Katika mchezo huo Milango ilikuwa migumu mpaka mapumziko kutokana na safu ya ulinzi ya timu zote kuonekana kuwa imara.

Kipindi cha pili, timu zote zilifanya mabadiliko huku kila mmoja akihitaji ushindi ili aweze kujiweka katika mazingira mazuri ya kufuzu michuano hiyo.

Kiungo wa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Feisal Salum (kushoto), akimtoka mchezaji wa timu ya taifa ya Guinea, katika mchezo wa pili wa kufuzu michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Kundi H, uliocheza jana kwenye Uwanja wa Charles Konan Banny, Yamoussoukro nchini Ivory Coast. Stars ilishinda goli 2-1.

Mabadiliko hayo yalizaa matunda kwa timu ya Taifa Stars, ambapo dakika 61 Feisal Salum aliachia mkwaju mkali nje ya 18 na kuifungia timu yake goli la kwanza huku goli la pili likitiwa kimiani na Mudathir Yahaya dakika ya 89.

Goli la kufutia machozi kwa timu ya Taifa ya Guinea, lilifungwa na Mohamed Bayo dakika ya 57 baada ya kumzungusha beki wa Stars Ibrahim Abdallah ‘Bacca’.