October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara, Ludovick (aliyevaa miwani) akitembelea Banda la Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) katika Maonesho ya Nanenane yaliyofunguliwa leo katika viwanja vya Nyakabindi mkoani Simiyu. .

NDC yashauri wakulima Kanda ya Ziwa kuchangamkia fursa za kilimo

Na Mwandishi Wetu, Simiyu

SHIRIKA la Taifa la Maendeleo NDC limewata wananchi wa mikoa ya Kanda ya ziwa ikiwemo Simiyu, Mwanza, Geita na Shinyanga, kujitokeza kwa wingi katika Maonesho ya Nane Nane ambayo yamefunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ili kuchangamkia fursa mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo ikiwemo katika uboreshaji wa sekta ya kilimo.

Wito huo umelewa leo na Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa NDC, Innocent Msuha mara baada ya maonesho hayo ya Nane Nane mwaka huu kufunguliwa rasmi.

Miongoni mwa fursa ambazo, Msuha amewataka wakazi wa mikoa ya Kanda ya ziwa kuchamkia ni pamoja na ukopeshaji wa matrekta kwa wakulima wadogo ambao utawasaidia katika kuinua uzalishaji wa mazao na kuijenga Tanzania ya viwanda.

“Sisi Kama NDC tunaona namna pekee ya kumwinua mkulima wa kitanzania Ni kumpatia mkopo wa trekta ambao hauna riba na kwa gharama nafuu,tunahesimu jembe la mkono limetutoa mbali lakini ni wakati muafaka umefika wa kuliweka makumbusho na sisi Kama shirika tumedhamiria kufanya hivo,” amesema.

Kupitia mradi huu wakulima hupata fursa ya kukopeshwa trekta ambalo huunganishwa na kiwanda cha shirika hilo kilichopo Kibaha mkoani Pwani ambapo mpaka sasa zaidi ya matrekta 550 yameshatolewa kwa wakulima katika mikoa mbalimbali hapa nchini.

Licha ya fursa ya matrekta fursa nyingine iliyoko ndani ya NDC ni pamoja na wananchi wa mikoa ya Kanda ya ziwa kuweza kujipatia dawa za kupambana na mazalia ya mbu maarufu kama Biolavicides ambazo pia zinapatokana katika maonyesho haya.

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara, Ludovick, akitembelea maonesho ya Nane Nane leo

“Vita dhidi ya mbu vimepiganwa muda mrefu lakini tunashindwa kufanikiwa kwa sababu badala ya kupambana na chanzo cha malaria tunapambana na mbu mpevu na ndio maana NDC kupitia kiwanda chake cha viuadudu kilichoko Kibaha mkoani Pwani kimeamua kuja na muarobaini wa kuhakikisha kuwa tunapambana na chanzo Cha Malaria kwa kutumia teknolojia pekee ya viuadudu ambayo inapatika Tanzania pekee katika bara zima la Afrika”

Msuha amesema endapo wananchi wa mikoa ya Kanda ya ziwa watachangamika fursa ya kutumia dawa hizo watakuwa wameepukana na janga la magonjwa yanayosababishwa na mbu ikimo malaria, zika, chikungunya, dengu ambayo yanachangia kupoteza nguvu kazi ya taifa kila uchwao.

Aidha fursa nyingine ambayo wananchi wanaweza kuitumie ni pamoja na kununua mashine na vipuli mbalimbali kupitia katika kiwanda cha NDC cha KMTC ambacho kinapatikana Moshi mkoani Kilimanjaro.

Mashine hizo ni pamoja na za kulanda mbao, kukoboa na kusaga pamoja na vipuli mbalimbali vya mashine ambavyo wakati mwingine hulazimika kuagizwa na kutengenezwa nje ya nchi.

NDC ni shirika kongwe hapa nchini ambalo lipo tangu enzi za ukoloni na liliasisiwa rasmi na Serikali mwaka 1962 likiwa na lengo la kuchochea na kuboresha maendeleo nchini ambalo kwa sasa kwa mujibu wa walaka wa baraza la mawaziri wa mwaka 1996 limepewa jukumu la kuendeleza miradi ya kimkakati pamoja na kuendeleza sekta ya Viwanda hapa nchini.