October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamishna wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Mstaafu Thomas Mihayo akizungumza kwenye mafunzo ya wasimamizi wa uchaguzi majimbo na maafisa ugavi katika Ukumbi wa Moyo wa Huruma Mjini Geita. (Picha na Mutta Robert, TimesMajira Online).

NEC: Wasimamizi shirikisheni vyama vya siasa kuepuka dosari Uchaguzi Mkuu 2020

Na Mutta Robert,TimesMajira Online, Geita

Kamishna wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji mstaafu Thomas Mihayo amewataka wasimamizi wa uchaguzi kuhakikisha wanashirikisha vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi ili kuepuka mchakato huo kuingia dosari.

Amesema kuwa, maeneo yote ambayo vyama vya siasa vinatakiwa kushirikishwa wasimamizi washirikishe vyama hivyo pamoja na wadau wengine wa uchaguzi katika maeneo yao.

Jaji Mihayo ameonya kuwa,kama wasimamizi hao wa uchaguzi wasiposhirikisha vyama vya siasa itasababisha uchaguzi huo kuleta malalamiko na kuwa na matatizo.

Wasimamizi wa uchaguzi,wasimamizi wasaidizi wa majimbo na maafisa ugavi wakiwa kwenye mafunzo ya siku tatu katika ukumbi wa Moyo wa Huruma mjini Geita. (Picha na Mutta Robert, TimesMajira Online).

Kiongozi huyo wa NEC amesema hayo katika mafunzo kwa wasimamizi wa uchaguzi,wasimamizi wasaidizi wa majimbo na maafisa ugavi kutoka mkoa wa Kagera na Geita yaliyofanyika katika ukumbi wa Moyo wa Huruma mjini Geita yatakayofanyika kwa siku tatu mfululizo.

Jaji Mihayo amewataka wasimamizi kufanya kazi za uchaguzi kwa kufuata katiba ya nchi,sheria za uchaguzi,kanuni za uchaguzi,maadili ya uchaguzi pamoja na muongozo ya NEC.

Aidha, ameonya wasimamizi wa uchaguzi wasitumie uzoefu katika uchaguzi bali wafuate katiba ,sheria ,kanuni na maadili ya uchaguzi.

Msimamizi wa uchaguzi wa Manispaa ya Bukoba, Limbe Maurice amesema kuwa katika manispaa hiyo,wamejipanga kufanya kazi kwa kutenda haki kwa wagombea wote bila kupendelea yeyote.

Naye msimamizi wa uchaguzi wa Wilaya ya Nyang’hwale, Mariam Chaurembo amesema kuwa, katika wilaya hiyo,NEC imeshawapa mafunzo mengi hivyo wamejipanga kuhakikisha uchaguzi unakuwa huru na haki.

Ameongeza kuwa,katika uchaguzi huo watatenda haki kwa wagombea wote bila kupendelea mgombea yoyote na watazingatia katiba,sheria ,kanuni na maadili ya uchaguzi.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi inaendelea na maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa udiwani, wabunge na Rais unaotarajiwa kufanyika Oktoba 28, mwaka huu.