September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Barabara ya Pangani-Saadan-Bagamoyo Km 256 kukamilika 2025

Na Hadija Bagasha, Timesmajira Online,Pangani

Serikali imesema hadi ifikapo mwaka 2025 barabara ya Tanga Pangani , Saadan – Bagamoyo yenye urefu wa km 256,itakuwa imekamilika pamoja na daraja la mto Pangani ambapo mpaka sasa wakandarasi wapo eneo la mradi ‘site’ na kazi zinaendelea.

Mradi wa ujenzi huo wa barabara ya unaounganisha mikoa ya Tanga na Pwani kupitia Bagamoyo ukikamilika unatajwa kwenda kufungua fursa za kiuchumi, usafiri na usafirishaji katika mwambao wa Tanga,mikoa ya jirani pamoja na Nchi jirani ya Kenya.

Huku wawekezaji wengi wa ndani na nje ya nchi wameanza kuingia wilayani Pangani mkoani Tanga kwa ajili ya kutafuta maeneo ya uwekezaji wa hoteli, viwanda, na biashara nyingine baada ya uwekezaji uliofanywa na serikali wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Tanga Pangani yenye urefu wa kilomita 50 na daraja la mto Pangani lenye urefu wa mita 525.

Akizungumza mara baada ya kutembelea mradi wa barabara ya Tanga Pangani na mradi wa daraja la mto Pangani akiwa ameambatana na Baraza la wazee kutoka jijini Arusha Mjumbe wa Kamati kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM),Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Tanga Rajab Abrahaman Abdalah amesema kuwa uwepo wa mradi huo unakwenda kufungua uchumi wa Mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

“Kabla ya barabara hii Pangani ilikuwa kama kisiwa,lazima uje kwa sababu maalumu uje uzike au kwenye harusi lakini sasa inakuja kufunguka kiuchumi ndio maana wawekezaji wengi wa ndani na nje ya nchi wanaendelea kuja hapa kuwekeza, “amesisitiza Rajab.

Katibu Mkuu Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania Askofu Daktari Israel Masa Ole Gabriel amepongeza kazi zinazofanywa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkoa wa Tanga wamejionea miradi mbalimbali waliopitishwa.

“Tumejionea kule ambako tumekwenda kwenye kituo cha kupokea mafuta kutoka Uganda,tumeona mapango ya Amboni na hapa pia ambako tumeona barabara na daraja,serikali sisi viongozi wa dini tuna kila sababu ya kuwaunga mkono, “ameeleza Askofu OleGabriel.