September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wachezaji 124,kutimua vumbi mashindano ya Gofu

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

JUMLA ya wachezaji 124 wakiwemo 52 wa kulipa na 72 wa ridhaa wamesajiliwa kushiriki mashindano ya Gofu kwaajilii ya kumuenzi mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya wanawake gofu,marehemu Lina Nkya yatakayotimu vumbi katika viwanja vya gofu Gymkana mkoani Arusha.

Hii ikiwa raundi ya tatu ya mashindano hayo ambayo yameanza kurindima leo katika viwanja hivyo vya Gymkana.

Akizungumza mara baada ya kumaliza kufanya usajili, Mchezaji wa kulipwa Nuru Mollel amesema kuwa amejipanga vizuri kwa ajili ya mashindano hayo na anamatarajio makubwa ya kuhakikisha kuwa anaibuka mshindi.

Amesema anawaomba watanzania kujitokeza kuja kuona kile wanachokifanya na kwamba anawapongeza wale wote waliowezesha mashindano hayo kufanyika kwa weledi na ubora wa hali ya juu.

“Nimejipanga vizuri hasa katika kuhakikisha naibuka mshindi katika mashindano haya, hata hivyo kushiriki kwenye jambo hili kwangu mimi ni fursa hasa ya kukutana na wachezaji wenzangu na kuendelea kubadirishana uzoefu,” amesema Mollel

Naye mchezaji ambaye ni mshindi wa ridhaa kwa raundi mbili za mashindano hayo ambazo ni Morogoro na Moshi, Alli Sanzu amesema mashindano hayo ya Arusha ni ya muhimu kwake kwa sababu ni ya mwisho kuelekea kwenye mashindano makubwa nchini Dubai.

Amesema amewekeza nguvu zake zote katika mashindano hayo kuhakikisha anafanya vizuri na kuibuka mshindi.

Mashindano hayo raundi ya kwanza yalifanyika Mkoani Kilimanjaro ya pili mkaoni Morogoro na Sasa ni Mkoani Arusha ambayo Julai 10,2024 usajili wa wachezaji wa gofu wa mashindano hayo ulifanyika katika viwanja hivyo vya gofu Gymkana Mkoani Arusha.

Mashindano hayo yatafanyika kuanzia Julai 11 hadi 14, 2024 ambapo siku ya mwisho ya mashindano hayo shughuli nzima ya kugawa zawadi kwa washindi wote kwa hatua zote zitafanyika na mshindi wa kwanza atajipatia kikombe na pesa taslimu .

Mshindi wa Mashindano ya kwanza kwa msimu huu yaliyofanyika Viwanja vya TPC Moshi mkoani Kilimanjaro alikua Moreli akifuatiwa na Fadhili Nkya , kwa yaliyofanyika Mkoani Morogoro mshindi wa kwanza alikua Hassan Kadio na katika nafasi ya pili ni Abdalah Yusuph.