October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CPA Makalla amtaka Mkandarasi kukamilisha Mradi kabla ya 2025

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Dar

KATIBU wa NEC, Siasa, itikadi, Uenezi na mafunzo CCM Taifa, CPA Amos Makalla, ambaye pia ni Mlezi wa Chama cha CCM Mkoa wa Dar es Salaam, amewataka Wakandarasi kukamilisha miradi kwa wakati, hususani mradi wa maji wa Bangulo ulio katika Jimbo la Ukonga Wilaya ya Ilala, kabla ya mwakani, ili wananchi waweze kunufaika na mradi huo kwa wakati.

Makalla ameyasema hayo leo, Julai 7, 2024 Jijini Dar es Salaam, akiwa kwenye ziara yake alipotembelea mradi huo wa mkubwa wenye thamani zaidi ya Bilioni 36, ukiwa na ujazo wa Lita Milioni 9, ambao utachukua Maji kutoka Ruvu juu na kuhudumia katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es salam ikiwa pamoja na Kinyerezi, Kipunguni, Mwanagati, Ilala na Temeke.

“Nitoe wito kwenu nyie Wakandarasi mliopewa tenda katika mradi huu, huu ni mradi mkubwa na unaenda kunufaisha wananchi katika maeneo korofi kwa maana ya maeneo yenye ukosefu wa maji katika Jiji la Dar es Salaam, hivyo naomba ukamilike kwa wakati kabla ya kufika mwakani kwani sisi kazi yetu ni kuhudumia wananchi katika kuwaletea miradi ya maendeleo”, amesema Makalla.

Aidha, Makalla amempongeza Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kumtua Mama ndoo kichwani kufuatia Mradi huo, huku akieleza kuwa, una kwenda kumaliza shida ya maji Dar es salam.

Pia, amempongeza Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, kwa kazi nzuri anayoendelea kufanya ya kuhakikisha anapeleka huduma ya maji katika maeneo mbalimbali ikiwa pamoja na kuwaondoa wakandarasi wanaochelewesha ukamilikaji wa miradi.