September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ulega azindua taarifa ya 21 ya hali ya uchumi (Sekta ya mifugo) nchini

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amezindua taarifa ya 21 ya hali ya uchumi wa Tanzania iliyoandaliwa na Benki ya Dunia ambayo awamu hii imeangazia eneo mahususi la sekta ya mifugo.

Ulega amezindua taarifa hiyo mapema leo Juni 24, 2024 jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine amesema taarifa hiyo imeipongeza Serikali ya awamu ya Sita, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa jitihada za makusudi inazozichukua kuhakikisha sekta hiyo inakuwa na kuendelea kutoa mchango mkubwa kwa pato la taifa.

Miongoni mwa masuala ambayo yameangaziwa katika taarifa hiyo ni pamoja na serikali kuongeza bajeti ya sekta ya mifugo ambayo imewezesha sekta kuboresha miundombinu ya uzalishaji na masoko, kuweka miundombinu ya mashamba ya mifugo na mbegu, udhibiti wa magonjwa na kuimarisha huduma za ugani.

Aidha, taarifa hiyo imeonesha pia umuhimu wa kuongeza uwekezaji katika sekta hiyo hususan kwa kushirikisha sekta binafsi ambao wamekuwa na mchango mkubwa katika kukuza sekta hiyo hapa nchini.

Taarifa hiyo ambayo huwa inaandaliwa na Benki ya Dunia kuhusu hali ya uchumi kwa sekta tofautitofauti hutolewa mara mbili kila mwaka na awamu hii imeangazia sekta ya mifugo hapa nchini.