October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

BAKWATA yazindua mradi wa kuchochea maendeleo ya jamii Mwanza

Na Daud Magesa, Timesmajira Online, Mwanza

BARAZA Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA),limezindua mradi wa kuchochea maendeleo ya jamii mkoani Mwanza unaolenga kukusanya bilioni 2.2 kwa mwaka ulioenda sambamba na Baraza la Eid Al Adh’aa.

Akizindua mradi huo Juni 18,2024 Sheikh wa Mkoa wa Mwanza,Alhaji Hasani Kabeke amesema utakakuwa shirikishi unaolenga kubadilisha fikra za waislamu na wasio waislamu ili kuleta maendeleo.


“Umasikini si ucha Mungu wala siyo dini,kupitia mradi huu wa AHLUL KHAYR (Watu wa Kheri),lengo ni kubadilsisha fikra kwa waislamu na wasio waislamu kuleta maendeleo,hivyo tunatafuta watu 10,000 watakaotuunga mkono kuleta maendeleo bila kujali imani zao za dini,”amesema.

Sheikh Kabeke amesema tangu kuanza kwa zoezi hilo, tayari wamepata ahadi ya milioni 1.37 na kuwaomba watu wa imani mbalimbali za dini kuwaunga mkono kwa kuchangia sh. 1000 kwa mwezi ili kutimiza lengo walilojiwekea la kukusanya bilioni 2.2 wanazokusudia ambapo wadau watakaochangia watakuwa na maamuzi fedha hizo zifanye nini.

Awali Ustaadhi Hamis Butije amesema kipaumbele cha mradi huo wa kuchochea maendeleo ya jamii mkoani Mwanza utakaokuwa na awamu tatu ni ujenzi wa vituo vya afya katika Wilaya saba mkoani humo,tayari Wilaya za Ilemela na Sengerema zimekamilisha majengo ya wagonjwa wa nje (OPD) ya vituo hivyo vipya.

Amesema katika uchangiaji wa fedha wameweka makundi yatakatochangia sh.1000 watu 7000 kwa mwezi sawa na milioni 84 kwa mwaka,kundi lingine litachangia sh.2000 kwa mwezi sawa na milioni 48 kwa mwaka,watu 1000 wao watachangia sh.3000 kwa mwezi sawa na sh.milioni 36 kwa mwaka.

Ustaadhi Mtije ameeleza kuwa makundi mengine yatachangia sh.5000 kwa mwezi na kuingiza sh. milioni 30 kwa mwaka,jingine litakalochangia sh.10,000 hilo litaingiza sh.milioni 60 kwa mwaka na kufanya jumla ya sh. bilioni 2.219.

“Zikipatikana hizo sh. bilioni 2.219 kutokana na watu 184,000 ambao ni asilimia 5 ya idadi ya wakazi milioni 3.6 wa Mkoa wa Mwanza,miradi hiyo ya kuchochea maendeleo ya wananchi katika sekta ya afya ambayo ni shirikishi itakamilika,”amesema.

Aidha BAKWATA kama mdau wa maendeleo itatumia sehemu ya fedha hizo kusaidia yatima na wengine wenye mahitaji ya kibinadamu,kununua vifaa tiba,dawa na kuandaa rasilimali watu hivyo changamoto ya ajira kwa baadhi ya vijana inaweza kupungua kupitia mradi huo wa kiuchumi.

Naye Meneja Rasilimali Watu na Utawala wa kampuni ya GPB Tanzania Ltd, Yakubu Mussa amesema“Nikupongeze Sheikh Kabeke kwa maono lakini ia kuwaunganisha waislamu na wasio waislamu mkoani Mwanza,niwaombe viongozi wa dini endeleeni kuliombea taifa letu na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan,ameweka mazingira mazuri kwa wafanyabiashara kufanya biashara,hivyo malengo hayo ya maendeleo yakizingatiwa mtadika mbali,”amesema.