October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaipongeza TSIA kwa kutimiza miaka 20

Na Mwandishi wetu,Timesmajira Online

Serikali imekipongeza Chama cha Sekta Binafsi ya Ulinzi Tanzania (TSIA) kwa kutimiza miaka 20 na kutoa ajira kwa vijana wapatao elfu tatu na kupunguza wimbi la vijana wanaojiingiza katika shughuli zisizo rasmi zikiwemo za kiuhalifu.

Hayo yamebainishwa Juni 19,2024 katika hotuba ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa iliyosomwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Daniel Sillo (Mb) katika ufunguzi wa mkutano mkuu wa kazi wa 16 wa TSIA jijini Dodoma.

“Mmefanya kazi nzuri ya uwekezaji wa ndani katika sekta ya ulinzi wa watu na mali zao, nawapongeza kwa kuwa na uhusiano mzuri na vyombo vingine vya ulinzi na usalama mnashirikiana vizuri na Jeshi letu la Polisi sanjari na Jeshi letu la Zimamoto na Uokoaji,”ameeleza Sillo a kuongeza kuwa;

“Wananchi mnaowahudumia, wameweza kuwatumia walinzi wenu kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu wenyewe, hivyo suala la uaminifu na utunzaji wa siri ni jambo muhimu katika kupambana na uhalifu ninaomba tuzingatie sheria za nchi hususani sheria za haki za binadamu, kuna mazoea ya watu kujichukulia sheria mkononi kwa kuwaadhibu wahalifu kwa kisingizio cha hasira kali, vitendo hivi vinapingana na dhana nzima ya utawala bora wa sheria,”.

Ameeleza kuwa chama hicho kina dhamana kubwa kwa wateja wao na kinahitaji nidhamu na uvumilivu wa hali ya juu kwa kuangalia namna ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi ili kuleta tija katika utendaji kazi wa kila siku kwani bila kuwa na maslahi mazuri, watendaji wengi hujikuta wakifanya kazi wakiwa wamekata tamaa.

Hivyo ni rahisi kwao kurubuniwa na kujiingiza katika vitendo vya kiuhalifu pia kumeku na uwepo na taarifa ya baadhi ya walinzi wa kampuni kujihusisha katika njama za uhalifu wengine wakidiriki kuazimisha silaha kwa kisingizio cha kuporwa.