October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nchimbi ataka wenye roho za wizi,ubadilifu kuombewa

Na Hadija Bagasha, Timesmajira Online, Tanga

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa Balozi Dkt. Emanuel Nchimbi ametoa wito kwa wananchi kuwaombea watu wenye roho za wizi na ubadhilifu ili fedha hizo ziweze kukidhi matarajio ya Watanzania.

Dkt Nchimbi aliyasema hayo Juni 7, mwaka huu wakati wa mapokezi yake yaliyofanyika eneo la Mombo wilayani Korogwe akitokea mkoani Kilimanjaro.

“Mtu anatakiwa kuweka mifuko 10 ya saruji yeye anaweka miwili huko ni kuhujumu tuwaombee watu wenye roho za wizi, roho za ubadhilifu ili waache na Tanzania iweze kukamilisha miradi yake kwa ufanisi,”amesema Dkt.Nchimbi.

Pia ameeleza kuwa wapo viongozi Afrika ambao wanakwenda kutafuta fedha halafu wanagawana wenyewe yeye na familia yake lakini sio kwa Rais Samia ambaye amejipambanua kuhakikisha nchi inapiga hatua kimaendeeo.

Kuhusu ombi la Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini Timotheo Mnzava aliyetaka Mji wa Mombo upate hadhi ya halmashauri kamili, Balozi Dkt Nchimbi amesema atashirikiana na uongozi wa serikali kuhakikisha mji huo unapata hadhi hiyo ili na yeye awe sehemu ya historia.

Katika hatua nyingine Dkt.Nchimbi amempokea aliyekuwa Katibu wa Chama cha Wananchi (CUF) Wilaya ya Korogwe Vijijini Nurdin Abubakar ambaye aliamua kurudi Chama cha Mapinduzi ili kuweza kusaidia kuchochea kasi ya maendeleo kwa kushirikiana na viongozi waliopo madarakani.

Awali akizungumza katika mkutano huo,Mbunge Jimbo la Korogwe Vijijini Timothea Mzava amesema wakati Rais Samia anaingia madarakani bajeti ya TARURA ilikuwa ni milioni 690 leo ni zaidi ya bilioni 2.3 barabara zinajengwa na kukarabatiwa ikiwemo Mombo na upande wa afya amekamilisha Hospitali ya Wilaya ya Korogwe .

Pia amesema vimejengwa vituo vya Afya vinne na zahanati zaidi ya 10 huku akieleza kwa upande wa elimu hawana changamoto ya madarasa watoto wanasoma.

Rais Dkt Samia Suluhu ametoa kiasi cha shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ujenzi wa bwawa kubwa la umwagiliaji la Mkomazi ambalo Mkandarasi tayari ameanza kazi na wanaamini litakapokamilika litakuwa mkombozi kwa wananchi wa Tarafa ya Mombo.

“Katika suala la maji wakina Mama wametuliwa ndoo kichwani ambapo ametoa bilioni 3 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa mradi wa maji wa Mji wa Mombo na jana Mkandarasi amekabidhiwa kazi kwamba changamoto chache azibebe ili chama izisukume,”.

Hata hivyo amesema wiki mbili alitangaza kutokuunga mkono bajeti ya ujenzi ili kuishiniza Serikali itoe majibu kuhusu kujengwa kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Korogwe-Dindiri,Bumbuli mpaka Soni.

” Ni ya muda mrefu na wametangaza inakwenda kuanza ujenzi nikiombe chama kiisukume serikali ili ahadi hiyo iliyomo kwenye ilani ya CCM, itekelezwe,”.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga Rajab Abdallah alimhakikishia kiongozi huyo kwamba kutokana na kasi aliyofanya Rais ya kuwaletea maendeleo deni lao kubwa ni kuhakikisha wanachukua vitongoji 572 vyote vilivyopo mkoani humo, mitaa yote 263 na vijiji 779.