October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

IGP.Wambura:Uhalifu,wahalifu havina nafasi

Judith Ferdinand, Timesmajira Online, Mwanza

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Camillus Wambura,amewavisha Nishani Maofisa, Wakaguzi na Askari wa vyeo mbalimbali wa Kanda ya Ziwa kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan huku akieleza kuwa jeshi hilo limedhamiria kuhakikisha amani inatawala na kusisitiza kuwa uhalifu na wahalifu havina nafasi ndani ya nchi yetu.

Nishani hizo walipewa na Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambapo kwa Kanda ya Ziwa wamepewa nishani hizo Maofisa 22,wakaguzi 5 na askari wa vyeo mbalimbali 5.

IGP.Wambura amebainisha hayo Mei 24,2024 jijini Mwanza wakati wa hafla ya kuwavisha Nishani Maafisa, wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali iliyofanyika uwanja wa Polisi Mabatini ambapo amewasisitiza kuendelea kutekeleza mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai kwa kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja.

“Hatutarudi nyuma na kuacha wahalifu wanatamba ndani ya nchi yetu,” amesisitiza IGP Wambura.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Said Mtanda amelipongeza Jeshi la Polisi nchini kwa namna linavyofanya kazi na kuhakikisha amani na utulivu unatawala.

Naye Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Wilbrod Mutafungwa kwa niaba ya makamanda wa Polisi Kanda ya Ziwa amesema nishani zilizotolewa na Rais zimeongeza morali na uwajibikaji kwa kwenda kusimamia misingi itakayoleta mafanikio.