October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Viongozi wastaafu wamkuna JPM mkutano CCM, aanika mafanikio

Joyce Kasiki na Doreen Aloyce, TimesMajira Online, Dodoma

MWENYEKITI wa CCM Taifa, Rais John Magufuli amefungua Mkutano Mkuu chama hicho huku akionesha furaha yake kuwaona viongozi wakuu wastaafu wakihudhuria mkutano huo wakiwemo Mawaziri Wakuu wastaafu Edward Lowasa na Fredrick Sumaye.

Mbali na hilo ametumia fursa hiyo kuelezea mafanikio machache yaliyofanywa na chama hicho kwa kipindi cha miaka mitano, huku akiwashukuru wanaCCM kwa kushirikiana naye kutekeleza mafanikio hayo.

Rais Magufuli ambaye ndiye Rais anayemaliza mhula wake wa kwanza wa miaka mitano  akitarajia kuwania tena nafasi hiyo,Oktoba mwaka huu  amesema wajumbe na wananchi kwa ujumla ndio  mashahidi wa namna ambavyo nchi imepiga hatua kimaendeleo.

“Ninyi nyote ni mashahidi jinsi ambavyo tumetekeleza miradi ya Barabara,afya,umeme, nchi yetu kufikia uchumi wa kati, ujenzi wa reli ya treni SGR na  mambo mengine.

Mafanikio haya yametokana na watangulizi wangu akina Mzee Ali Hassan Mwinyi,Benjamini Mkapa na Jakaya Kikwete na wanaCCM kwa ujumla, kila mmoja alitimiza wajibu wake katika kuitengeneza Tanzania,” amesema Rais Magufuli.

Kauli ya Mwenyekiti wa TLP

Mwenyekiti wa Chama cha TLP, Augustino Mrema amesema kutoka na utendaji kazi wa Rais Magufuli, kampeni za chama hicho zitakuwa ni za kumwombea kura za ndiyo kwa wananchi.

Hata hivyo Mrema aliomba chama chake kipate uwakilishi katika bunge na kata.

“Sisi hatugombei urais kwa sababu haina maana ya kufanya hivyo, kwani Magufuli anatosha, lakini ombi langu naomba nipate wawakilishi bungeni na kwenye kata.” Amesema Mrema

Lowassa

Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Lowassa amesema hakuna ubishi kuwa nchi inetulia kutokana na uongozi thabiti wa Rais Magufuli hadi uchumi umepaa.

“Naomba spidi hiyo isipungue,” amesema Mrema.

Silinde

Aliyekuwa Mbunge wa Momba kupitia CHADEMA na baadaye kuhamia CCM, David Silinde amesema ameridhishwa kwa asilimia 100 namna ambavyo CCM ipo imara.

” Pia nineridhishwa na utendaji wa Rais Magufuli ,tutayasema haya nchi nzina ,CCM ina sifa kubwa ya kuthubutu na kuchukua hatua lakini pia kutekeleza kwa vitendo maendeleo ya Watanzania.

CCM ni chama kikubwa hakilingani na chochote ,tutazunguka kila mahali kueleza CCM inavyofanya kazi .”Alisema Silinde.

Kinana

Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM, Abdulrahman Kinana aliwaomba wajumbe kumpa Rais Magufuli kura zote za ndiyo ili apate faraja na nguvu ya kuongoza Taifa.

Aidha amewataka wanachama wa chama hicho kuwa na mshikamano hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi Mkuu kwa kujitolea kutafuta kura za Magufuli,wabunge na madiwani.