October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanahabari wajitokeza kuwania Jimbo la Mufindi Kaskazini

Na Zuhura Zukheir, TimesMajira Online, Iringa

JOTO la uchaguzi likiendelea kupamba moto hapa nchini wanahabari mkoani Iringa wamkalia kooni mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini Mahmoud Mgimwa baada ya kujitokeza na kutangaza nia ya kuwania jimbo hilo kupitia chama cha mapinduzi ccm

wanahabari hao Agustino Kihombo na Sebastian Atilio kwa nyakati tofauti wameliambia gazeti hili kuwa wamejipima na kuona wanatosha kuwatumikia wananchi wa jimbo la Mufindi Kaskazini kama katiba ya chama inavyoleza.

mwanahabari Agustino Kihombo ambaye ni kada wa CCM amewaomba wananchi wa Jimbo la Mufindi Kaskazini kumpokea kwani ni kijana aliyezaliwa na kusoma katika kijiji cha Itona ndani ya jimbo hilo.

Aidha kada huyo wa Chama cha Mapinduzi na mwanahabari Agustino Kihombo alisema kama chama chake kitampa ridhaa ya kuwa mgombea anaenda kuleta fikra mpya na maendeleo endelevu kwa wana-Mufindi Kaskazini japo hakutaka kuviweka wazi vipaumbele vyake na kusema muda utakapofika ataweka wazi.

Kwa upande wake mwanahabari Sebastian Atilio alisema kuwa umefika wakati wa mabadiliko katika jimbo kwa kuchagua vijana.

Atilio ambaye anenda na kauli mbiu ya siasa safi,kazi na sala anasema anazijua changamoto za wana-Mufindi kaskazini hivyo kama CCM itampa ridhaa ataenda kutatua changamoto hizo ambazo aliahidi kuzitaja muda ukifika.

Watia nia wa chama cha mapinduzi wataanza kuchukua fomu za kuwania kuteuliwa ifikapo Julai 14,mwaka huu.

Kwa upande wake mwanahabari Victor Meena ambaye ni kada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)a yeye ametangaza nia ya kugombea Jimbo la Kalenga ambalo mbunge wake alikuwa Godfrey Mgimwa.

Meena ambaye ni mwanahabari mbobezi wa masuala ya kijamii alisema baada ya kuwatumikia wananchi kwa njia ya kalamu na kusikia kilio chake sasa naona ipo haja ya kuwatumikia kwa kuwakilisha kilio chao bungeni.

Alisema kama chama chake kitampa ridhaa ya kugombea atakwenda kuleta mageuzi kwa wana-Kalenga ambao muda mrefu wameshindwa kufahamu mbunge wao yupo wapi.

Meena anasema wakati huu ni sahihi kwake kwenda kuwatumikia wana-Kalenga ili kurudisha hadhi ya jimbo hilo lenye historia ndani na nje ya nchi.