September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais wa IFAC atembelea Tanzania

Na Mwandishi wetu, Timesmajira Online DSM

Rais wa Shirikisho la Wahasibu duniani (International Federation of Accountants-‘IFAC’) Asmaa Resmouki atembelea Tanzania kwenye kongamano la Wahasibu la mwaka 2023 lililofanyika katika viwanja vya APC Bunju Dar es salaam kuanzia tarehe 29/11/2023 hadi 1 Disemba 2023.

Asmaa Resmouki ni mwanamke wa kwanza kushika nafasi hiyo ya Urais wa shirikisho la Wahasibu duniani.

Tanzania ikiwakilishwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imekuwa mwanachama wa shirikisho la Wahasibu toka mwaka 1986

Tanzania imenufaika kwa ujio wa wa Rais huyo kwani ni fursa kubwa kuelezea maendeleo ya Taaluma ya Uhasibu nchini na changamoto zake kwa lengo la kuipeleka Taaluma hiyo mbele.

Tanzania kupitia NBAA imekuwa ni nchi ya pili kutembelewa na Rais huyo barani Afrika toka kuchaguliwa kwake.

Katika kongamano hilo la Wahasibu, NBAA na wanachama wake imefanya mbio za hisani kwa ajili ya kuchangia matibabu ya watoto wanaosumbuliwa na saratani katika hospitali ya Muhimbili na kufanikiwa kukusanya kiasi cha sh. Milioni kumi na tano ( 15,000,000/-) na kukabidhi hospitalini hapo siku ya tarehe 30/11/2023.

Awali akizungumza kabla ya kukabidhi hundi, Mkurugenzi Mkuu wa NBAA, CPA Pius Maneno amesema kila mwaka wana utaratibu wa kurejesha kwa jamii kwa mwaka huu wameona ni vema wakawagusa watoto wanaoumwa saratani ambao wamelazwa hospitali ya Taifa Muhimbili.

Sambamba na hilo limefanyika zoezi la kuchangia damu kwa wahitaji kama sehemu ya kurudisha kwa jamii.