October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Idadi ya simba yaongezeka nchini

Na Queen Lema times majira Arusha

Imeelezwa kuwa bado Tanzania ni nchi yenye idadi kubwa ya Simba duniani ambapo mpaka sasa wapo zaidi ya 17,000 ikiwa idadi hiyo imeongezeka kutoka 16,000 awali.

Hayo yameelezwa jijini Arusha na Mkurugenzi Mkuu wa TAWIRI, Dkt. Ernest Mjingo Novemba 30,2023 wakati akiongea na vyombo vya habari juu ya tafiti mbalimbali ambazo zinafanywa na taasisi hiyo lakini pia maandalizi ya kongamano la 14 la Kisayansi ambalo linatarajiwa kuanza Arusha Desemba 6 mpaka 8 mwaka huu.

Dkt Mjingo amesema kuwa TAWIRI wameweza kuhesabu Simba wote ambao wapo ndani ya hifadhi mbalimbali nchini hapa ambapo kuna ongezeko.

Amefafanua kuwa hapo awali Simba waliokuwepo walikuwa 16,000, ila kwa mujibu wa tafiti ambazo wanezifanya zimeweza kubaini kuwa kuna Simba 17,000.

“Mojawapo ya kazi ya zetu ambazo tunazifanya ni pamoja na kupata idadi ya wanyama na kwa simba tayari tumeshapata idadi hiyo na bado tunaendelea kutoa na kufanya tafiti mbalimbali,”ameongeza.

Katika hatua nyingine amesema kuwa tafiti ambazo zinafanywa na TAWIRI zina manufaa makubwa kwa jamii hasa kwa wadau wa utalii endapo tu kama wanafuatilia kwa karibu juu ya tafiti hizo.

“Sisi ni watafiti na kwa sasa kila mara huwa tunatoa matokeo ya utafiti mbalimbali ambao tunafanya tunatangaza hata aina mpya ya utalii ni muhimu sana kuanzia sasa wadau wa utalii kuhakikisha kuwa wanaangalia hizi tafiti zitawasaidia sana,”amesema.

Pia amesema kuwa ili kujua matokeo ya tafiti hizo ambazo zimekuwa zikifanywa na TAWIRI ni muhimu sana kwa wadau wa utalii kuweza kujumuika na wanasayansi katika kongamano la 14 la kisayansi.