October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TAKUKURU yabaini upotevu wa wastani wa sh.380,000 kila siku stendi ya 88

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Dodoma  imebaini uwepo mianya ya Rushwa katika stendi ya magari yaendayo  mikoani ya Nane Nane jijini Dodoma  ambapo wastani wa shilingi 380,000 hupotea kila siku.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake kuhusu utekelezaji wa shughuli za robo ya pili ya mwaka ,Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Dodoma Sostenes Kibwengo amesema,kiasi hicho cha pesa kupotea kila siku ni sawa na shilingi milioni 130 kwa mwaka.

“Hizi ni fedha nyingi ambazo zinaweza kufanya maendeleo makubwa katika nchi lakini zikiachwa bila kufuatiliwa na kuzibwa kwa mianya inayosababisha upotevu wa fedha hizo huigharimu nchi na wananchi kwa ujumla.”amesema Kibwengo na kuongeza kuwa

“Kwa hiyo katika kuhakikisha tunaziba mianya hiyo rushwa,tulifanya uchunguzi wetu ambapo tumebaini chanzo cha upotevu huo na tumeendelea kutoa elimu ili kuzuia mianya hiyo ya rushwa kwani lengo ni kudhibiti kabla upotevu wa fedha haujatokea.”Amesema

 Aidha amesema,TAKUKURU Mkoani Dodoma imeokoa sh milion 296.5 za miradi ya maendeleo katika halmashauri mbalimbali huku akisema imefuatilia miradi ya maendeleo 49, yenye thamani ya sh bilion.7 katika halmashauri za mkoani Dodoma.

“Katika ufuatiliaji wetu tumebaini mapungufu mbalimbali ambayo yanajitokeza,ikiwemo wananchi kutokatiwa risiti za makusanyo ya fedha kupitia mashine za kielektroniki za kukusanyia mapato (POS) ambapo watendaji wamekuwa wakikaa na fedha mkononi badala ya kuziwasilisha benki kama sheria inavyosema.

Kwa uapnde wa miradi alisema kuna mapungufu ya usimamizi wa miradi hiyo kitendo ambacho kinachangia kwa kiasi kikubwa upotevu wa mali za serikali.

Amewataka watendaji kuwa mstari wa katika kusimamia ipasavyo miradi ya maendeleo inayotekelezwa lakini pia amewataka wananchi kufuatilia miradi mbalimbali inayotekelezwa katika maeneo yao na kutoa taarifa pindi wanapoona kuna viashiria vya rushwa.