September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watatu wakamatwa kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya Mhadhili wa Chuo Kikuu SAUT

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online,Mwanza

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa watatu kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya Hamida Mussa, mwenye umri wa miaka 64, Mhadhili wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT) tawi laMwanza na mkazi wa Buzuruga.

Aliyeuawa kwa kunyongwa shingoni na nguo (mtandio) akiwa nyumbani kwake,ambapo inadaiwa kwamba, Novemba 28,2022 kuanzia asubuhi hadi Novemba 29,2022 mchana ndugu na marafiki wa marehemu Hamida Mussa kwa nyakati tofauti walikuwa wakitaka kufanya mawasiliano na ndugu yao bila mafanikio kwani simu yake ya mkononi ilikuwa ikiita bila kupokelewa hivyo wakaingiwa na wasiwasi hivyo waliamua kutoa taarifa kituo cha Polisi.

Akizungumza mkoani hapa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa, alisema kuwa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na viongozi wa Serikali ya mtaa walifika kwenye makazi ya Hamida Mussa nakukuta mlango ukiwa umefungwa huku nyumba ikiwa na ukimya ambao haukuwa wa kawaida.

Mutafungwa alieleza kuwa Hamida Mussa alikuwa anaishi na binti wa kazi aliyefahamika kwa jina moja tu la Sara,kutokana na hali hiyo waliamua kuvunja mlango na walipoingia ndani walimkuta mwanamke huyo akiwa amepoteza maisha kwa kunyongwa huku mwili wake ukiwa sakafuni na binti wa kazi akiwa ametowekakusikojulikana.

Alieleza kuwa,baada ya taarifa hizo ufuatiliaji wa tukio hilo ulianza kufanyika ikiwa ni pamoja na kumsaka msichana wake wa kazi ambapo Novemba 30,2022 muda wa saa 7 na dakika 30(13:30) mchana huko katika stendi ya mabasi wilayani Misungwi askari wakiwa kwenye ufuatiliaji wa mauaji hayo walimkamata Sara MwendeshaSahani, mwenye umri wa miaka 15, mkazi wa Ishokela Wilaya ya Misungwi aliyekuwa mfanyakazi wa nyumbani kwa marehemu akiwa na vitu mbalimbali alivyodai kuwa ni mali za marehemu alizozichukua mara baada ya kufanya tukio la mauaji.

Alitaka vitu alivyokutwa navyo baada ya upekuzi ni simu aina ya Tecno kitambulisho cha kazi, kadi ya bima ya afya, kadi ya benki ya CRDB, kadi ya mpiga kura, kadi ya Eco water, kadi ya posta , kitabu kidogocha kutunzia kumbukumbu vyote vikiwa na majina ya marehemu Hamida Mussa kasamuro.

Vile vile, mtuhumiwa amekutwa akiwa na pete mbili rangi ya dhahabu, mkufu mmoja rangi ya dhahabu,viatu, sabuni ya unga kilogramu 15, hereni moja, viberiti bunda 14, sabuni aina ya B29 boksi mbili , sukari kilogramu mbili, mabegi matatu makubwa na moja dogo la mgongoni yote yakiwa na nguo mbalimbali zamarehemu pamoja na nguo za Hamida Petro ambaye ni mjukuu wa marehemu.

Mutafungwa alisema,baada ya mtuhumiwa kuhojiwa kwa kina, ameieleza Polisi kuwa vitu hivyo vyote alivichukua kutokanyumbani kwa marehemu baada ya kuwa amemuua kwa kumnyonga shingo Novemba 28,2022, kisha kujifungia naye ndani.

Ambapo ilipofika Novemba 29,2022 alitoroka akiacha amemfungia kwa ndani marehemu ambapo mtuhumiwa ameendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kueleza kuwa aliamua kufanya tukio hilo kwa sababu ya hasira kwa kuwa marehemu alikuwa akimkaripia anapofanya makosa hapo nyumbani.

Pia alikuwa akimpiga makofi na kumpa kazi ngumu na katika purukushani za kumkaba marehemu binti huyo anadai aling’atwa kwenye kidole chake cha kati cha mkono wa kulia na kweli amekutwa na jeraha.

Hivyo baada ya kutenda unyama huo, mtuhumiwa aliondoka na vitu vya marehemu alivyokamatwa navyo hadi Misungwi ambako alimpigia simu mama yake mzazi aitwaye Mashiri Benard anayeishi kijiji chaIshokela ili ampatie baadhi ya vitu kama zawadi, mama huyo alifika na kupatiwa baadhi ya vitu hivyo nakurejea kijijini.

Hata hivyo, ameeleza kuwa vitu vingine alikwenda kuvihifadhi nyumbani kwa Tabu zumbe Seleman ambaye ni shemeji yake aishiye Misungwi.

Aidha Kamanda huyo wa Polisi ameeleza kuwa watuhumiwa watatu ambao ni Sara Mwendesha Sahani,Mashiri Benard mwenye umri wa miaka 43, mkazi wa Ishokela na Tabu Zumbe Selemani, wamekamatwa kwa hatuazaidi za kisheria.

Ambapo ukamataji huo umetokana na operesheni kali na misako inayoendelea mkoani hapa yenye lengo la kutokomeza uhalifu na wahalifu wote.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linaendelea na uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo kabla ya kuwafikisha watuhumiwa Mahakamani.