October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TAKUKURU yaokoa milioni 9.8/- za halmashauri

Na Peter Ringi TimesMajira Online, Simanjiro

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Simanjiro mkoani Manyara imeokoa jumla ya sh.milioni 9,800,000 mali ya halmashauri hiyo zilizokuwa mikononi mwa wazabuni.

Ilielezwa kuwa, wazabuni walipokea fedha hizo kwa ajili ya kufanya manunuzi ya vifaa vya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Simanjiro, hawakuwasilisha vifaa hivyo hadi mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Yefred Myenzi alipoomba msaada wa TAKUKURU ili fedha za umma ziweze kurejeshwa.

Aidha, kwa kutumia taasisi hiyo ndipo fedha hizo kiasi cha milioni tisa na laki nane ambazo zilitaka kupotea zikarejeshwa na wazabuni hao wanaofahamika kama Shidchwa Enterprises and Logistics ya Dar es Salaam pamoja na MAURA ya mkoani Iringa.

Baada ya wazabuni hao kukamatwa na kuhojiwa na maafisa wa TAKUKURU walikiri kupokea fedha hizo za halmashauri na kuomba kuzirudisha na ndipo walipozirudisha fedha hizo kwa kupitia akaunti ya TAKUKURU alibainisha Mkuu wa taasisi hiyo Mkoa wa Manyara,Holle Makungu.

Kwa mujibu wa Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Manyara, Holle Makungu amesema, fedha hizo ni kwamba kiasi cha sh.7,064,000 zilikuwa zimepewa mzabuni wa Kampuni ya Shidchwa Enterprises and Logistics ambapo zingine zilipokelewa na MAURA.

Wakati huo huo huko wilayani Simanjiro, TAKUKURU inamshikilia mmiliki wa shamba la mtu anayefahamika kwa jina la Thomas Meliyo kwa kutowalipa watumishi wa shamba lake lenye ukubwa wa ekari zaidi ya 200.

Imeelezwa kuwa, Mihayo ameajiri vijana wapotao 23 ambao kazi yao ni kupanda, kupalilia, kupukuchua mahindi na kupiga maharage huku wakiishi kambini ambako kuna uhaba mkubwa wa maji uliowafanya wasionge kwa takribani miezi sita huku wakiamriwa kunawa uso pekee. Tayari tasisi hiyo imeanza kufanyia kazi malalamiko ya vijana hao.