September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Songa wamkabidhi Mwana FA koroboi, ndoo, majembe

Na Steven William,TimesMajira Online. Muheza

WAKAZI wa Kitongoji cha Paratembo Kata ya Songa wilayani Muheza, wamemkabidhi taa za kibatari na ndoo za maji mgombea Ubunge Jimbo la Muheza, Hamisi Mwinjuma ‘Mwana FA’ wakionesha ishara ya kwamba wana kero ya shida ya umeme na maji katika kitongoji hicho.

Tukio hilo limetokea juzi baada ya wananchi hao kusimamisha msafara wa mgombea ubunge huyo wakati akitokea katika mkutano wa kampeni Kijiji cha Kwakibuyu Kata ya Songa.

Wakazi hao baada ya kusimamisha msafara huo, wamemkabidhi mgombea huyo kibatari, ndoo tupu za maji na majembe ya kulimia wakionesha ishara kwamba wanataka huduma ya umeme, maji na
wana uhaba wa ardhi ya kulima mashamba kwani ardhi yote imechukuliwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) pamoja na wageni.

Kwa upande wake, Mwana FA amepokea taa hiyo ya koroboi, ndoo za maji tupu na majembe ya kulimia.

Amesema anatambua changamoto zote katika kata nzima ya Songa, ikiwamo shida ya maji, wanataka umeme, shida ya ardhi ya kulima mashamba, ukosefu wa barabara bora, ukosefu wa zahanati na shule za
msingi kuwa na upungufu wa madarasa, vyoo na uhaba wa walimu.