June 27, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NMB, UNCDF wafungua njia mpya kwa kampuni changa za kidijitali


Na.Mwandishi wetu,Timesmajira

Benki ya NMB na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) wamesaini Hati ya Ushirikiano inayolenga kuimarisha mazingira ya kuibua, kukuza na kupanua kampuni changa zenye mawazo bunifu ya kidijitali kupitia uwezeshaji wa kisera na kisheria, masoko, mitaji na ushauri wa kitaalamu.

Makubaliano hayo yamesainiwa jijini Dar es Salaam na Afisa Mkuu wa Teknolojia na Mabadiliko ya Kidijitali wa Benki ya NMB, Kwame Makundi, pamoja na Katibu Mtendaji wa UNCDF, Pradeep Kurukulasuriya. Ushirikiano huo unaendeleza Programu ya PesaTech, iliyoanzishwa mwaka 2022 na ambayo tayari imeziwezesha kampuni changa 22 za teknolojia ya fedha.

Makundi amesema kampuni tano tayari zinafanya kazi na NMB, huku tatu zikiunganisha huduma zake katika NMB Mkononi Super App. Benki hiyo inalenga kuingiza zaidi ya kampuni changa 30 katika mfumo wake ifikapo mwaka 2030 na kuziunganisha na mitaji, masoko, wataalamu na mifumo ya kidijitali.

Kurukulasuriya amesema UNCDF inaiona NMB kuwa mshirika muhimu katika kukuza kampuni changa na kuyageuza mawazo bunifu kuwa biashara zenye uwezo wa kuongeza ajira na kutatua changamoto za wananchi.