March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Fyandomo mguu kwa mguu Mbeya,kusaka kura za wagombea wa CCM

Na Esther Macha Timesmajira Online, Mbeya

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Suma Fyandomo, ameendelea na kampeni ya mguu kwa mguu kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa kushiriki katika uchaguzi mkuu  Oktoba 29, 2025 na kuchagua wagombea wa chama hicho.

Fyandomo ameshirikiana na wagombea wa nafasi za Ubunge wa chama hicho wa majimbo yote mkoani humo, akiwahimiza wananchi  umuhimu wa kuchagua viongozi wanaotokana na CCM.

Amekuwa akizungumza na wananchi  moja kwa moja kwa kuwafuata katika maeneo yao ikiwemo sokoni, vijiweni, kwenye maduka ya nyama, saluni za kike, gereji, vilabu vya pombe za kienyeji pamoja na  wajasiriamali wadogo.

Ambapo ametumia fursa hiyo kuwaelezea wananchi hao namna  ilani ya uchaguzi ya CCM 2020–2025  iliyotekelezwa  na  malengo mapya kuelekea  ilani ya 2025–2030.

“Tunaona maendeleo  yaliyofanywa na Serikali  chini ya  CCM katika sekta za afya, maji, barabara, elimu na nishati vijijini na mijini,”.

Hivyo amewaomba wananchi hao kumpigia kura Dkt Samia Suluhu Hassan kwa nafasi ya urais, wabunge na madiwani wanaotokana na CCM na kuwataka kutokubali kurubuniwa na maneno ya chuki.

Pia Fyandomo, amewahimiza wananchi kudumisha amani na mshikamano ikiwemo  wanawake na vijana, madereva wa bodaboda, bajaji, mama lishe na baba lishe.