Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online
KAMPUNI ya Mawasilino ya Yas kwa kushirikiana na Mixx, imezindua rasmi maandalizi ya mbio za Yas Zanzibar International Marathon 2025.
Mbio hizo zinatarajiwa kufanyika Novemba 23, 2025, chini ya kauli mbiu ya “Kila Hatua ni Special.”.
Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo uliofanyika Oktoba 16, Meneja Mawasiliano na Uhusiano YAS, Christina Murimi alisisitiza umuhimu wa mbio hizo katika kuhamasisha afya, utalii, na maendeleo ya jamii kupitia teknolojia na ushirikiano endelevu.
“Kauli mbiu yetu inabeba ujumbe kwamba kila hatua tunayopiga iwe ni mbio, maamuzi ya maisha, au juhudi binafsi ina thamani yake. Kila hatua ni fursa ya kujifunza, kukua, na kubadilisha maisha,” amesema Murimi.
Mbio za mwaka huu zitakuwa 5KM, 10KM, na 21KM, ambapo washiriki wote watajisajili na kulipia kupitia mfumo wa kidigitali wa Mixx.
Jambo hilo linarahisisha usajili na kuhakikisha kila mshiriki anapata taarifa muhimu, ikiwemo uthibitisho wa usajili, namba ya mbio, na ratiba ya siku ya tukio.

Kwa upande wake Kiongozi wa Mbio hizo Ali Said aliongeza kuwa “Mara zote tunapopanga mbio hizi, lengo letu ni kuunda tukio linalowaunganisha watu wa kila umri na hali ya maisha.
“Tunaamini kila mshiriki anaposhiriki, anakuwa sehemu ya hadithi kubwa ya Zanzibar – ya afya, mshikamano, na maendeleo.”
Aliongeza kuwa, mbio hizo hazina maana ya michezo tu, bali pia ni tukio linalounganisha michezo, teknolojia, na utamaduni wa Zanzibar, likiwa kivutio cha utalii wa michezo ndani na nje ya visiwa.

Alitoa wito kwa wananchi wote vijana, wanawake, familia, na wageni kujisajili mapema kupitia mtandao wa Mixx by Yas ili kushiriki katika tukio hili la kipekee.
YAS inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya kidigitali nchini, ikiwemo mtandao wa 4G na 5G unaofika Unguja na Pemba, kuhakikisha kila Mzanzibari anapata nafasi sawa ya kufikia dunia ya kidigitali.
Kupitia mbio hizo, kampuni inathibitisha kuwa teknolojia inaweza kuwa chachu ya afya, utalii, na maendeleo endelevu ya jamii.
Watanzania wote wanashauriwa kujisajili mapema na kushiriki kwa wingi katika mbio za Yas Zanzibar International Marathon 2025, zinazotarajiwa kufanyika tarehe 23 Novemba.
Tukio hilo la kipekee ambalo linalounganisha michezo, utalii, na teknolojia linafanyika kwa kauli mbiu ya “Kila Hatua ni Special”, likiwapa washiriki fursa ya kushuhudia na kuwa sehemu ya hadithi kubwa ya Zanzibar.

More Stories
Usajili wa Laini za Simu: Jilinde Dhidi ya Kutumiwa Vibaya kwa Utambulisho Wako
TTCL yaadhimisha siku ya Wanawake kwa kutoa msaada JKCI
Wananchi Dodoma washauri TBA kujenga nyumba za kupangisha watu binafsi