April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampuni ya Swissport Tanzania yasaini mkataba wa miaka mitatu na Taasisi ya CCBRT

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

KAMPUNI Ya Swissport Tanzania imesaini mkataba wa miaka mitatu na Taasisi ya CCBRT ambapo Swissport Tanzania itatoa shilingi milioni 40 kwa miaka mitatu kwa ajili ya matibabu ya watoto waliozaliwa na changamoto ya miguu vifundo

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Jana, Mkurugenzi Mkuu wa Swissport Tanzania Mrisho Yassin amesema, wametengeneza mazingira mazuri na CCBRT kwa kuwa wadau wazuri wa kuchangia shughuli zinazofanywa na Taasisi hiyo na kuvutiwa na namna huduma zinavyotolewa hasa katika kuwahudumia watoto waliozaliwa na matatizo ya viungo.

“Tunafurahi kwasababu tumetengeneza mazingira mazuri na CCBRT, tumekuwa wadau wazuri wa kuchangia shughuli zinazofanywa na CCBRT, tumepata nafasi ya kutembelea hapa na tukavutiwa na shughuli zinazofanywa na CCBRT, kwa namna ambavyowanawahudumia watoto waliozaliwa na matatizo ya viungo”

“Kila mwaka tutatoa kiasi cha fedha kwaajili ya kuwasaidia matibabu ya watoto hawa na Mkataba wa miaka mitatu na tutakuwa tunatoa kiasi Cha shilingi milioni 40 Kila mwaka katika kusaidia matibabu ya watoto wanaozaliwa na matatizo ya viungo”

Aidha Mrisho ameipongeza CCBRT kwa jitihada kubwa wanayoifanya katika kusaidia jamii na kuahidi kuendelea kushirikiana nao.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya CCBRT Brenda Msangi amesema makubaliano hayo ya miaka mitatu yataenda kuwasaidia watoto wengi wenye tatizo la mguu kifundo kwa kwenda kubadilisha maisha yao.

“Milioni 40 kwa Kila mwaka inamaanisha kwamba kuna watoto 50 wenye tatizo la mguu kifundo tunaenda kubadilisha maisha yao, bado kuna watoto hawapati matibabu haya na wanaendelea kubaki na Ulemavu wa kudumu ambao unaweza kutibika na kuwa msaada kwenye jamii”

Msangi amesema Watoto wanaozaliwa na mgongo kifundo Kila mwaka nchini Tanzania ni takribani watoto 2400, ambapo matibabu yake huchukua takribani miaka mitano huku kila mwaka wanapokea watoto wapya takribani 400.

Kutokana na hivyo, Msangi ametoa rai kwa wadau mbalimbali kuendelea kutoa ufadhili kwenye Taasisi ambazo zinatoa matibabu hayo ili kuhakikisha kwamba watoto wanaozaliwa na tatizo hilo waweze kupata matibabu.

“Rai yangu ni kwamba tunahitaji wadau wengi zaidi kuendelea kutoa ufadhili kwenye Taasisi ambazo zinatoa matibabu haya ili kuhakikisha kwamba watoto wanaozaliwa na tatizo hilo wasiachwe nyuma, aweze kupata matibabu”

Pia amewataka wazazi wanaowapeleka watoto wao wenye tatizo hilo la mguu kifundo kutokatisha matibabu yao ili kuepusha mtoto anapata huduma iliyo kamili na kuweza kuondokana na tatizo hilo.

“Watoto wengine wanakuwa wanaanza kupewa matibabu lakini yanaishia katikati, inawezekana kwasababu mzazi anakosa nauli, miguu ikianza kuonekanika imekaa sawa saa nyingine wazazi wanaacha kuwaleta wale watoto kuendelea na matibabu kwahiyo mtoto anapata kurudi kwenye hali aliyopo”

“Watoto wengine wanakuwa wanaanza kupewa matibabu lakini yanaishia katikati, inawezekana kwasababu mzazi anakosa nauli, miguu ikianza kuonekanika imekaa sawa saa nyingine wazazi wanaacha kuwaleta wale watoto kuendelea na matibabu kwahiyo mtoto anapata kurudi kwenye hali aliyopo ambayo inaukuwa ni gharama zaidi kurekebisha huo mguu”

Mbali na hayo Msangi amesema wanaendelea kutoa elimu kwa mabalozi wao, vyombo vya Habari na wagonjwa wenyewe ambao walishapona ili kuhakikisha wanapokutana na mtoto mwingine mwenye tatizo hilo aweze kwenda kituo Cha afya na kupatiwa matibabu.

“Siyo watu wote wanaelewa kwamba hili tatizo linarekebishika, na ni tatizo la kiafya, hivyo sisi kama CCBRT jambo la kwanza huwa tunatoa elimu hata kwa kutumia mabalozi wetu Tanzania nzima, vyombo vya Habari na wagonjwa wenyewe ambao walishapona wanakuwa mabalozi wakubwa kuhakikisha kwamba wanapokutana na mtoto mwingine mwenye hili tatizo anaenda kwenye kituo cha afya ambacho kinatoa matibabu haya”

Aidha ameishukuru Swissport Tanzania kwa kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo ambapo awali walitoa mashine ya Ultrasound ambayo hadi sasa imesaidia watanzania wengi.