September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Baadhi ya Wazee wakimsikiliza Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi (hayupo Pichani) wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wazee Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Nyerere Square Mjini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WAMJW)

‘Zungumzeni na watoto wenu wazingatie maadili ya ndoa’

Na Steven Augustino,TimesMajira Online. Tunduru

WAZEE wamehimizwa kuzungumza na watoto wao wazingatie maadili ya ndoa, ili waishi na waume na wake zao kwa kuvumiliana zikiwa ni juhudi za kuwapunguzia wazee kulea wajukuu, ambao wamekuwa wakitelekezwa baada ya watoto wao kutendana.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Tunduru, Richard Mbambe aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Julius Mtatiro kwenye maadhimisho ya Siku ya Wazee Duniani yaliyofanyika kwenye Ukumbi wa Klasta ya Walimu wa Tarafa ya Mlingoti.

Amesema endapo wazee hao wataendelea kuachia tabia za kuoana na kuachana ziendelee kuota mizizi, vijana wao watashindwa kutimiza wajibu wao wa kuawahudumia.

Mbambe pia ameitaka jamii kutimiza wajibu wao wa kuwalea wazee na kwamba hayo yatafikiwa, endapo wazee hawatoa msukumo kwa watoto wao kusoma, kufanya kazi yoyote ya kuwaingizia kipato.

“Utasikia vijana wanalalamika kuwa vyuma vimekaza, lakini kukicha asubuhi utawakuta wanacheza bao, hawajishighulishi na kazi yoyote mchana akirudi nyumbani anakuta kawekewa ugali, wanyimeni chakula watapata akili ya kujishughulisha,” amesisitiza Mbambe.