September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watakiwa kutekeleza malengo ya serikali kuleta mabadiliko ya kidijitali

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

KATIBU Mkuu wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mohammed Khamis Abdulla amewasihi vijana walionufaika na ufadhili wa mafunzo ya muda mrefu awamu ya pili kupitia mradi wa Tanzania Digital (DT) kutumia fursa hiyo kutekeleza malengo ya Serikali yakuongeza wabunifu katika mabadiliko ya Kidijitali nchini.

Abdulla amesema hayo jijini hapa leo, Julai 12,2024,katika hafla ya kutoa vyeti na kutia saini Mkataba wa kutumikia Serikali baada ya kumaliza Masomo kwa Watalaam wa Tehama waliopata ufadhili kupitia Mradi wa Tanzania ya Kidijitali huku akisisitiza kufuata wanachoendea na kuwakumbusha kuwa serikali imewalipia kwenda kusoma na siyo mkopo.

“Mtambue kuwa chanzo pekee cha mafanikio ni ujuzi na uzoefu hivyo basi mkasome kwa bidii na kupeperusha bendera ya taifa letu la Tanzania kwa uzalendo mkubwa na kulinda maslahi ya Taifa “,amesema.

Aidha amesema kuwa wao kama Wizara tayari wamekamilisha masuala ya maboresho kwa kuendelea kufanyia baadhi ya mifumo ikiwa ni pamoja na kukamilisha mkakati wa miaka 10 wa uchumi wa Kidijitali unaolenga ujuzi wa jamii ya Kidijitali.

“Ujuzi mtakaopata utusaidia taaluma yenu na kuwasaidia Watumishi wenzenu kubuni,kuelimisha na kusukuma gurudumu la mabadiliko ya Kidijitali,sisi kama Wizara tumekamilisha baadhi ya masuala mbalimbali tunaendelea kuyafanya, ” amesema

Mbali na hayo ameeleza kuwa kama Wizara wamekamilisha mkakati wa miaka 10 wa uchumi wa Kidijitali, unaolenga ujuzi wa jamii ya Kidijitali ambayo ni kuwa na jamii inayojua Teknolojia katika biashara na mambo mengine ya biashara mtandao. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa chanzo cha Diaspora kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Salvatory Mbilinyi akitoa mwogozo juu ya mambo wanayopaswa kufanya wawapo nje ya nchi amewaisitiza wanufaika wa mradi huo kutii na kufuata sheria za nchi pamoja na vyuo ambavyo wanaenda ili waweze kutimiza malengo yao kwa manufaa ya taifa, familia pamoja wao binafsi.

Vilevilea amewahimiza kuwa wavumilivu na changamoto zote kipindi wapo masomoni pamoja na kulinda tamaduni za kitanzania kwa kuzingatia maadili na siyo kujisahau wanapokutana na tamaduni za nje ya nchi.

Awali akitoa salamu kwa niaba ya Benki ya Dunia Mratibu wa mradi wa Digital Tanzania (DT), Bakari amesema kupitia mradi huo wanatengeneza vituo bunifu ambavyo vitaenda kuwasaidia wanafunzi wanaomaliza vyuo pamoja na walioko mtaani kuweza kusaidiwa kuendeleza na kuonesha uwezo wao walionao.

“Vilevile kupitia mradi huu wa DT tunaenda kutengeneza mifumo ambayo kila siku Mhe. Rais amekuwa akiuongelea wa jamii namba ambapo kila mtanzania inabidi awe na namba moja ambayo itamuwezesha kupata huduma kokote aendako”,amesema.

Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na utawala bora Ibrahim Mahumi amewataka wakafuate Sheria,Taratibu na Kanuni na kuongeza kuwa ni mategemeo ya Ofisi ya Raisi na Utumishi na Serikali kwa ujumla kuwa wanufaika hao watakapo kwenda masomoni watafanya kile ambacho kinakusudiwa kufanyika na sio Mambo mengine. 

Akitoa Shukurani kwa niaba ya wanufaika wote Mhandisi Mwandamizi kutoka mfuko wa mawasiliano kwa wote Brian Kasuma amesema kuwa watatumia fursa hii adhimu kwa kujibiidisha katika masomo ili kuweza kuchangia katika maendeleo ya nchi na hasa katika uchumi wa Kidijitali na kuahidi kuwa mabalozi wa kuitangaza Tanna vivutuo vyake.

“Tunaahidi kutumikia vyema fursa hii adhimu kwa kujibidiisha katika masomo ili kuweza kuchangia katika maendeleo ya nchi yetu hasa katika uchumi wa Kidijitali. Pia tunaahidi kuwa wazalenndo wa nchi yetu na mabalozi wazuri wa jamii ya nchi yetu kwa kutii sheria na taratibu nchi husika tunazoenda kusoma na kuvitangaza vivutio vyetu vya utalii kila tutakapopata nafasi”.

Pamoja na mambo mengine Wanufaika waliosaini Mkataba huo na kupokea vyeti kwa ni 30 ambapo ni awamu ya pili na awamu ya kwanza walikuwa 20 hivyo jumla wamefikia 50 ambapo ndio idadi iliyokuwa ikihitajika.