September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wananchi Mashewa wataka CCM itekeleze Ilani kwa kuwapatia maji

Na Yusuph Mussa, TimesMajira Online, Korogwe

WANANCHI wa Kijiji cha Kwetonge, Kata ya Mashewa, Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga, wamekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutekeleza ahadi zake zilizopo kwenye Ilani ya CCM ya 2020- 2025, ya kuwapatia maji.Waliyasema hayo kwa nyakati tofauti Februari 4, 2023 katikati ya sherehe za miaka 46 ya kuzaliwa chama hicho zilizofanyika kiwilaya Kijiji cha Kwetongo, ambapo mgeni rasmi alikuwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini Ally Waziri.

“Tangu tupate Uhuru kijiji chetu cha Kwetonge hakijapata maji ya bomba. Na hata zahanati yetu mpya ambayo imejengwa na Serikali huku wananchi wakichangia nguvu zao, haitaweza kufanya shughuli yeyote kwa vile hakuna maji.”

“Awali Serikali ilichimba maji ya kisima kirefu, lakini maji yake yakawa mabaya yana chumvi, na sasa imechimba kisima kingine maji mazuri yamepatikana, lakini maji hayo bado yapo ardhini, hayajajengewa miundombinu. Hivyo tunaomba Serikali iweze kutupatia maji” alisema Lucy Kisia mkazi wa Kijiji cha Kwetonge.

Naye Fatuma Kaghambe ambaye ni Mwenyekiti wa UWT Tawi la Kwetonge alisema wanawake wa kijiji hicho wanateswa na maji tangu Uhuru, hivyo wanaiomba CCM kuweza kuweka msisitizo kwa wataalamu wa maji kuweza kuwawekea maji ya bomba.Naye Nuru Ukoko ambaye ni Katibu wa CCM Tawi la Kwetonge alisema, tayari Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira (RUWASA) Wilaya ya Korogwe, wameshachimba kisima kirefu kwa mara ya pili, na wamepata maji baridi na yanafaa kwa matumizi ya binadamu, hivyo wanataka mchakato wa kujenga miundombinu ya maji uharakishwe.

“Dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kumtua ndoo kichwani mwanamke wa kijijini. Tunawataka wataalamu wa maji waweze kuja kuweka miundombinu ya maji ili kutimiza azma ya Mama Samia kwa wananchi kupata maji” alisema Ukoko.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe, Waziri, alimtaka Mhandisi wa RUWASA Wilaya ya Korogwe Joyce Malekela ambaye alikuwepo kwenye mkutano huo, atoe maelezo juu kero hiyo ya maji, ambapo alisema ni kweli wamechimba kisima kirefu cha maji kwenye kijiji hicho, na nia ni kujenga mradi wa maji kwa kuweka miundombinu.

“Ni kweli Kwetonge wana shida ya maji, lakini tayari RUWASA tumeanza mchakato wa kujenga mradi wa maji, ambapo tayari kisima kirefu kimechimbwa, na maji yamepatikana. Sasa tupo kwenye hatua za manunuzi, na mchakato huo unakamilika mwezi huu wa Februari, na ujenzi kuanza, na mradi utakamilika ndani ya miezi sita.”

“Mradi huo wa sh. milioni 600, utajengwa tenki lenye ukubwa wa lita 100,000, na kuwekwa vituo vya kuchotea maji (vilula) 11, huku maji hayo yakiwekwa kwenye taasisi za Serikali ikiwemo Zahanati ya Kijiji cha Kwetonge” alisema Malekela.

Waziri alisema, kupeleka fedha za miradi ni jambo moja, kutekeleza mradi ni jambo jingine, na kulinda miradi ni jambo jingine. Hivyo ametaka kuhakikisha fedha zinazotolewa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan zifanye kazi zilizokusudiwa kwa weledi.

Alisema baada ya mradi kukamilika, ni lazima wananchi wachangie huduma hiyo ya maji kwa kulipia, huku wao wananchi ndiyo wakiwa walinzi wa mradi huo kwa kuhakikisha miundombinu ya maji inalindwa.

“Msitumie maji hayo bure, na ni lazima mlipie maji hayo ili mradi uwe endelevu. Rais ameshatoa fedha za kuweza ninyi kupata maji, hivyo haiwezekani alete na fedha za kufanyia matengenezo ya mradi kwa vile Tanzania hii ni kubwa, kwani Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe yenyewe ina kata 29, vijiji 118 na vitongoji 610 . Na fedha za maji zisomwe kwa wakati ili wananchi waone fedha zao zipo salama.”

“Tuhakikishe tunalinda miundombinu ya maji kuona inakuwa endelevu. Asije akatokea mwananchi kuhujumu miundombinu au kukataa kuchangia maji, labda huyo mtu akaishi hewani, lakin sio hapa kijijini. Tunataka ushirikiano kuona miradi ya maji inakuwa endelevu, na wananchi wanaondokana na shida ya maji” alisema Waziri.

Waziri alisema miradi mingi ya maji imetekekezwa kipindi cha Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia, hivyo lazima miradi hiyo wailinde sababu ni ya fedha nyingi, huku akiwamwagia sifa Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tanga Mhandisi Upendo Lugongo, na Meneja wa RUWASA Wilaya ya Korogwe Mhandisi William Tupa.

“Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tanga na Meneja wa RUWASA Wilaya ya Korogwe ndugu yangu Tupa pamoja na wataalamu wa RUWASA, hawa wanafanya kazi kubwa na nzuri. Ukiangalia miradi iliyojengwa na inayoendelea kujengwa ukiwemo wa Mgwashi- Kwekibomi, Kwemasimba, Mombo- Mlembule, Sekioga, Makuyuni na Magila- Gereza, utaona imejengwa kwa kiwango” alisema Waziri.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri (kushoto) akipokea zawadi ya picha ya Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kutoka kwa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa UVCCM Wilaya, na Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Kijungumoto, Kata ya Mashewa Edward Katisho (kulia). Ni katika sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kiwilaya Kijiji cha Kwetonge, Mashewa Februari 4, 2023. Katisho pia alimkabidhi Mwenyekiti sh. 32,000 ili kununua mifuko ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya CCM Kata ya Mashewa. (Picha na Yusuph Mussa).
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri (kushoto) akitoa zawadi ya cheti kwa baadhi ya wanaCCM waliotoa mchango wao kwenye chama. Ni katika sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kiwilaya Kijiji cha Kwetonge, Mashewa Februari 4, 2023. (Picha na Yusuph Mussa).
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri akizungumza kwenye mkutano wa hadhara. Ni katika sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kiwilaya Kijiji cha Kwetonge, Mashewa Februari 4, 2023. Kulia ni Mhandisi wa RUWASA Wilaya ya Korogwe Joyce Malekela, ambaye alikuwa anajibu kero za maji kutoka kwa wananchi. (Picha na Yusuph Mussa).
Zahanati mpya ya Kijiji cha Kwetonge, Kata ya Mashewa ambayo imejengwa kwa fedha za wananchi na Serikali. Wananchi wanataka mradi wa maji uharakishwe ili maji yafike kwenye zahanati hiyo. Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri alifika kukagua ujenzi wake . Ni katika sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kijiji cha Kwetonge, Kata ya Mashewa Februari 4, 2023. (Picha na Yusuph Mussa).
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri (katikati mwenye kilemba), akipokea taarifa ya ujenzi wa Zahanati Kijiji cha Kwetonge, Kata ya Mashewa. Ni katika sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kiwilaya Kijiji cha Kwetonge, Mashewa Februari 4, 2023. (Picha na Yusuph Mussa).
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Korogwe Vijijini mkoani Tanga Ally Waziri (wa pili kushoto) akifungwa kilemba na wananchi, mara baada kufika Kijiji cha Kwetonge, Kata ya Mashewa kwenye sherehe ya miaka 46 ya CCM iliyofanyika kiwilaya Februari 4, 2023. (Picha na Yusuph Mussa).