April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wachimbaji wadogo nchini kutengewa maeneo yenye taarifa za kijiolojia

Na Anthony Ishengoma,TimesMajira Online, Kahama

MKUU wa Mkoa wa Shinyinga Dkt. Philemon Sengati amesema maonesho ya Biashara na Teknolojia ya Madini ni muhimu kwasababu mkoa wa Shinyanga una jumla ya viwanda 737 ukijumuisha viwanda vya vikubwa vya kati na vidogo ikiwemo pia uwekezaji mkubwa katika sekta ya madini yenye wachimbaji wakubwa na wadogo.

Naibu Waziri Wizara ya Madini Pof. Shukrani Manya, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mara Ally Salum Api wakiwa katika zoezi la kutembelea mabanda ya washiriki wa maonesho ya Biashara na Teknolojia ya madini Manispaa ya Shinyanga.

Dkt.Sengati ameewsema mkoa wa Shinyanga una viwanda vikubwa 21, viwanda vya kati 11 na viwanda vidogo 705 ambavyo vyote uzalisha bidhaa mbalimbali ambazo soko lake liko ndani na nje ya Mkoa wa Shinyanga.

Dkt. Philemon Sengati amesema hayo jana wakati wa ufunguzi wa maonesho ya Biashara na Teknolojia ya madini ambayo yanafanyika nje kidogo ya Manispaa ya Shinyanga kwa mara pili ya tangu maonesho haya kuanzishwa rasmi mwaka 2020 na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wakati huo Bi. Zainab Telack.

Dkt.Sengati ameongeza kuwa faida zitokanazo na maonesho aya ni kwa waajasiliamali wakubwa na wadogo kupata sehemu ya kuweka bidhaa au huduma ili wananchi waweze kupata fursa muhimu ya kujua huduma na masoko ya bidhaa zao.

Aidha ametaja faida nyingine kuwa kwa kipindi chote cha maonesho wajasiriamali watapata fursa ya kujua mahitaji halisi ya watu na aina ya bidhaa ambayo watu wanaitaji na kuwawezesha kuboresha viwango vya huduma na aina ya bidhaa ambazo watu wanazipendelea na hivyo kuwawezesha wajasiliamali kujua aina ya bidhaa ambazo wataendelea kuzitoa.

Naibu Waziri wa Madini Prof. Shukrani Manya mgeni rasmi katika Maonesho hayo alisema Serikali kwa kipindi cha miaka mitano ijayo itaendelea kuwahudumia wachimbaji wadogo kwa kuwatengea maeneo maalumu ya uchimbaji madini lakini pia itafanya maboresho kwa kuwatengea maeneo yenye taarifa za msingi za kijiolojia.

Aidha Prof. Manya ameongoza kuwa makampuni makubwa ya uchimbaji madini yawekeze pia katika kutoa huduma za jamii katika maeneo jilani na eneo la uwekezaji kwa kuzingatia vipaumbele vya Halmashauri tofauti na awali ambapo makampuni hayo yalikuwa yakitoa huduma ndongo kama kuchangia chumba kimoja cha darasa.

Naye Dkt. Meshaki Kulwa Mwenyekiti wa TCCIA mkoa wa Shinyanga ameiomba Serikali kufikilia upya suala la utoaji ruzuku kwa wachimbaji wadogo pamoja na wajasiliamali waliowekeza katika kubuni na kutengeneza mashine zinazosaidia wachimbaji wadogo kama vile mashine za kusaga mawe ya dhahabu kusaidiwa ili waweze kujiendeleza zaidi ikiwemo kupelekwa nje kwa lengo la kupata teknolojia mpya.

Naibu Waziri Wizara ya Madini Pof. Shukrani Manya, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Dkt. Philemon Sengati pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mara Ally Salum Api wakipata maelekezo ya teknolojia ya uchimbaji madini katika zoezi la kutembelea mabanda ya washiriki wa maonesho ya Biashara na Teknolojia ya madini Manispaa ya Shinyanga.

Rais wa Chama cha Wachimbaji wadogo Tanzania John Mina amesema kuwa sio kweli kwamba wachimbaji wadogo wanavamia maeneo ya watu hii ni kwasababu kuna watu wana maeneo na leseni ambazo zimekaa kwa zaidi ya miaka minane bila kufanyiwa chochote wakati vibali hivyo vina ukomo wa miaka minane.

Kwa mantiki hiyo Bw. Mina ameiomba serikali kuwafutia leseni wale wote wanye hati miliki na leseni za vitalu vya madini ambavyo vimekaa zaidi ya miaka kumi na kuyatoa maeneo hayo kwa wachimbaji wadogo kuendelea na kazi za uchimbaji madini.

Maonesho ya Biashara na Teknolojia ya madini yanaendelea Mkoani Shinyanga na yamefunguliwa jana kwa lengo la kutoa fursa kwa wawekezaji katika sekta ya madini na biashara kukutana na kupoata taarifa muhimu kuhusu soko na teknolojia ya madini hapa Nchini.