September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waathirika ndoa za utotoni Shinyanga walilia elimu

Na Penina Malundo, Timesmajira

WAATHIRIKA wa Ndoa za Utotoni Mkoani Shinyanga wamesema kuwa bado elimu ya masuala ya ndoa za utotoni na athari zake kwa wananchi wa mkoa huo hazijafika ipasavyo kutokana na matukio ya wasichana kuozeshwa katika umri mdogo kuongezeka.

Wamesema miongoni mwa mbinu ambazo wazazi wanazitumia sasa ni kuwalazimisha watoto hao wa kike kwenda kuishi na wanaume na wanapopata mimba ndipo ulazimisha kuwazozesha kwa kisingizio cha mimba aliyobeba na wao kushindwa kuishi na mtoto ambaye anamimba.

Akizungumza jana kijiji cha Busambilo Kata ya Chibe Mkoani Shiyanga katika Kituo cha Kulelea waathirika wa ndoa za Utotoni pamoja na wanaoishi katika mazingira magumu cha Agape Knowledge Open School,wakati wa Msafara wa Mtandao wa Kutokomeza ndoa za utotoni Tanzania (TECMN)ikiwa muendelezo wa ziara zake katika mikoa minne nchini.

Mmoja wa wasichana wa Kituo hicho,Amina Juma (siojinahalisi) amesema asilimia kubwa ya wazazi wa mkoa huo hususan katika maeneo ya vijijini bado wana tabia za kuwaozesha watoto wa kike kwa umri mdogo kutokana na tamaa za mali pamoja na mila na desturi.

Amesema yeye ni mmoja wa waathirika wa tukio hilo ambapo mzazi wake alikuwa anataka kumuozesha hili aweze kupata fedha hali ambayo ilimfanya kukimbia kwao na kwenda kuishi katika kituo hicho.

Amesema wazazi wengi waaamini kuwa watoto wa kike ni kitenga uchumi kwao jambo ambalo si kweli kwani waanahaki ya kupata elimu na muda utakapofika wa kuolewa wataweza kuolewa bila kushinikizwa.”Wazazi waelimishe kuwa watoto wa kike sio kitega uchumi,kwamba upitie kwa mtoto wa kike ndio uweze kufanikiwa hizo ni mila zisizofaa,”amesema.

Shuhuda wa Ndoa za Utotoni kutoka Kijiji cha Manyada Mkoani Shinyanga,Hadija Yasim (17) siojina halisi amesema yeye alipokuwa na miaka 15,mjomba wake alitaka kumuozesha ili kuweza kuwa tajiri.

Amesema baada ya kusikia kuwa anataka kumuozesha yeye aliamua kwenda kutoa taarifa polisi ambapo Askari walimchukua na kumpeleka katika kituo cha Agape.

”Pale kijijini kwetu asilimia kubwa ya wasichana waliokama mimi tayari wameolewa na nilikuwa naona namna waliyokuwa wanayapitia hivyo mimi sikuwa tayari kuingia katika ndoa kwa umri wangu huu,”amesema na kuongeza

”Sikuwa tayari kuolewa na pale nilikuwa naishi na babu yake hivyo nilipoona mjomba ananilazimisha kuolewa ndipo nilipoamua kwenda Polisi kushtaki ili asije kunipeleka kwa lazima kwa mwanaume,”amesema.

Amesema maisha ya kituo cha Agape kwao ni mazuri kuliko kurudi majumbani mwao ambapo wanawafanyia ukatili wa kijinsia wa kutaka kuwalazimisha kuolewa katika umri mdogo ambapo baadae tunakuja kukumbwa na athari kubwa za kiafya.

Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Kituo hicho ambaye pia ni Mlezi,John Mayola amesema wao kazi yao kubwa baada ya kuwapokea watoto hao ni kuwapa ushauri na nasaha watoto hao ili waone hivi vitu vipo na ni vibaya.

Amesema kwa mwaka upokea jumla ya watoto 57 kati yao wapo watoto wenye kesi ya mimba za utotoni pamoja na ndoa.”Kwa mwaka huu kuanzia Januari hadi sasa ambao watoto wenye mimba amepokea watoto watatu kati ya hao mmoja tayari amejifungua na mtoto wake anamiezi miwili,huku watoto wa ndoa za utotoni nimepokea watoto Tisa,”amesema.

Mayola amesema anatamani serikali itoe elimu kwa watoto wa kike kwani wazazi wanakuwa na mbinu za kuwashawishi watoto hao kutaka kuwaozesha na wanapokataa wanawalazimisha kwenda kwa mwanaume na kuishi nae ili aweze kubeba mimba kisha iwe rahisi kumuozesha.

Msafara huo wa TECMN umewakilishwa na Mashirika mbalimbali ikiwemo Msichana Initiative,Binti Makini,Plan International,MyLegacy,Medea pamoja na Theatre Arts Femist Group ambapo wanaelekea Mkoani Tabora.