September 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Viongozi vyama vya siasa watakiwa kutoingilia mchakato uboreshaji daftari la mpiga kura

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma
 
VIONGOZI wa Vyama vya Siasa na Waadau wa Uchaguzi wameaswa kuzingatia sheria za uchaguzi, kanuni za uboreshaji,  maelekezo ya Tume na kusimamia miiko na mipaka ya uendeshaji wa zoezi la uboreshaji daftari kwa kutoingilia mchakato mzima wa uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura.
 
Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi Jaji Mstaafu Mahakama ya Rufani Mbarouk Salim Mbarouk ametoa rai hiyo leo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano a Tume Huri ya Taifa ya Uchaguzi kuhusu uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura.
 
“Mawakala na viongozi wa vyama vya siasa na wadau wote wa uchaguzi kwa ujumla,nawasihi msiingilie mchakato wa uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura vituoni.”amesema Mwenyekiti huyo
 
Amesema, iwapo zitajitokeza changamoto yoyote,ni vyema wakatumia sheria ,kanuni na taratibu zilizopo kuwasilisha kwa Tume changamoto hizo ili ziweze kupatiwa ufumbuzi huku akisema kuwa ,kwa upande wao watazingatia katiba, sheria ya uchaguzi na kanuni zilizotungwa chini ya sheria katika zoezi hilo la uboreshaji wa daftari. 
 
Aidha ametyumia nafasi hiyo kuwahimiza wadau hao kupitia majukwaa yao ya kisiasa, kijamii, kitamaduni, kiimani na kiuchumi kuwakumbusha wananchi wajitokeze kwa wingi kujiandikisha na kuboresha taarifa zao kwenye daftari la kudumu la wapiga kura. 
 
Awali , Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Tume ya uchaguzi Selemani Mtibora amesema kwa mkoa wa Dodoma kuna vituo 2,721 vitakavyotumika kwenye uboreshaji kwa nwaka huu ikiwa ni ongezeko la vituo 37 katika vituo 2,684 vilivyotumika kwenye uboreshaji mwaka 2019/20.
 
Kwa mujibu wa Mtibora jmla ya wapiga kura 594,494 wanatarajiwa kushiriki zoezi hilo ambapo watakao kosa sifa wataondolewa kwenye daftari hilo huku akisema baada ya uboreshaji huo inatarajiwa kwamba, daftari litakuwa na jumla ya wapiga kura zaidi ya milioni 34.7.
 
“Idadi hii inaweza kuongezeka kwa kuw inawezekana wapo watanzania ambao walikuwa na sifa za kuandikishwa kuwa wapiga kura wakati wa daftari la uboreshaji mwaka 2019/20 lakini kwa sababu moja au nyingine hawakuweza kujiandikisha kuwa wapiga kura,” amesema Mtibora
 
Naye Mratibu wa uandikishaji Mkoa wa Dodoma Charles Mduma amevielekeza vyama vya siasa kuzingatia mafunzo na maelekezo yanayotolewa na tume yanl uchaguzi ili kila mtu atimize wajibu wake.