October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UVIKUWA waadhimisha siku ya mtoto wa Afrika

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online

Umoja wa vituo vya kulea watoto Tanzania (UVIKUWA )wameadhimisha siku ya mtoto wa Afrika Dunia kwa kufanya usafi Zahanati ya Buyuni wilaya ya Ilala, na kutoa misaada kwa jamii.

Madhimisho hayo yaliongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Vituo vya kulea Watoto Tanzania Kunubwa Ntapara, ambapo walifanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Zahanati ya Buyuni na kutoa sabuni kwa watumishi wa Zahanati hiyo pamoja na Wazazi wa Watoto waliofika Kliniki.

“UVIKUWA leo tumeadhimisha siku hii ya mtoto wa Afrika kwa kufanya usafi na kugawa sabuni kwa Wazazi waliofika Kliniki na watoto wao dhumuni letu UVIKUWA kuwa karibu na Jamii “alisema Kunubwa.

Mwenyekiti wa UVIKUWA Kunubwa aliitaka jamii kutoa taarifa za vitendo vya mmomonyoko wa maadili kwa watoto ikiwemo ukatili wa kijinsia ambayo wanafanyiwa watoto majumbani kila siku.

Aliwataka Wazazi kulea watoto katika misingi imara waweze kupata elimu bora kwani Taifa la kesho linawategemea hivyo Wazazi wana jukumu kubwa la kuwalea watoto wao.

Katibu wa UVIKUWA Tanzania Vicent Lugiko alisema taasisi hiyo siyo ya kiserikali inaisaidia Serikali kupinga vitendo vya ukatili ambapo alitoa wito kwa jamii wawe sambamba kufuata sera ya watoto na kuakikisha usalama na Ulinzi wa mtoto unapatikana katika nchi yetu.

Alisema Taasisi hiyo ilianzishwa mwaka 2017 ina matawi kila sehemu pamoja na wanachama zaidi ya 3000.